JSON Variables

Header Ads Widget

Responsive Advertisement

Alhamisi, 19 Juni 2025

RAIS DKT. SAMIA AMEDHAMIRIA KUIENDELEZA SEKTA YA MADINI-MAJALIWA

...................

 

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa uzinduzi wa kiwanda cha kwanza cha kisasa cha kuchenjua shaba ni ishara ya dhamira ya dhati ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuisimamia na kuendeleza sekta ya madini.

 

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa kiwanda hicho chenye uwezo wa kuchenjua tani 31,200 za mashapo ya shaba kwa mwezi kitaleta manufaa kwa Wana-chunya na Taifa kwa ujumla.

 

Amesema hayo jana (Jumatano Juni 18, 2025) alipomuwakilisha Rais Dkt. Samia katika uzinduzi wa kiwanda cha Mineral Access Systems Tanzania Ltd (MAST), kilichopo katika kata ya Mbugani, Chunya mkoani Mbeya.

 

“Uthubutu na ubunifu wa Rais wetu Dkt. Samia ndio uliochagiza kwa kiasi kikubwa maendeleo katika Sekta ya Madini, wawekezaji hawa wamekuja kwasababu ya mazingira mazuri ya uwekezaji”.

 

Aidha, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa Wizara ya Madini na Taasisi mbalimbali nchini ziendelee kusimamia wawekezaji ili wanapofanya shughuli zao wazingatie Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi ikiwemo kulipa kodi stahiki, kutunza mazingira katika maeneo wanapofanya shughuli zao. “Hakikisheni pia wanzingatia Usalama wa wafanyakazi na raia wanaozunguka maeneo ya uwekezaji”.

 

“Ninyi pia wamiliki wa viwanda na wawekezaji wote hakikisheni mnaendesha shughuli zenu kwa kuzingatia matakwa ya sheria na hasa kwenye utunzaji wa mazingira mkishirikiana na halmashauri wenyeji, kijiji na Wilaya”.

 

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa wito kwa wawekezaji kuweka kipaumbele cha ajira kwa wakazi wanaozunguka maeneo ya uwekezaji ikiwemo za kitaalamu na hata ambazo sio za kitaalamu.

 

 “Ametuambia mkurugenzi mtendaji ameanza na vijana takribani 200 lakini wapo pia ambao wanakuja kila siku na tunaamini atapanua wigo kuajiri, tunataka kuona vijana wa Chunya wakifanya kazi hapa”.

 

Naye, Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa amesema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho ni sehemu ya utekelezaji wa sera na sheria ya madini inayotaka kuhakikisha madini ya Tanzania yanachimbwa, yanachakatwa na yanaongezwa hapa hapa nchini kabla ya kuuzwa nje ili kupanua wigo wa fursa za kiuchumi.

 

Ameongeza kuwa kiwanda cha MAST ni moja kati ya viwanda tisa vilivyowekwa kwenye mpango wa kujengwa kwa ajili ya kuongeza thamani ya madini kabla ya kuuzwa nje. “Kiwanda hiki bado hawajafikia hatua ya kutengeneza bidhaa za mwisho lakini ndio mpango wao, watatengeneza mpaka chuma za kutengenezea waya za umeme na nyama zilizopo kwenye magari”.

 

Juhudi hizi ni sehemu ya mpango wa taifa wa kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa madini barani Afrika, na kuongeza uwezo wa kuuza bidhaa zilizoongezwa thamani badala ya malighafi.

 

Kwa upande wake Rais na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya MAST Dkt. Glendon Archer amesema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho ni mwanzo wa uchimbaji n uendelezaji wa sekta ya madini nchini Tanzania na kwamba kampuni hiyo inampango wa kujenga viwanda vingine Dodoma na Arusha.

 

“Tutaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania, Viongozi wa Serikali wametupa ushirikiano mkubwa sana na ndio maana tumefika hapa leo”.

 

Kiwanda hicho ni matokeo ya uwekezaji wa zaidi ya dola za marekani milioni 10.

 

(Mwisho)

 

0 comments:

Chapisha Maoni

Listen Mkisi Radio