JSON Variables

Showing posts with label Top Stories. Show all posts
Showing posts with label Top Stories. Show all posts

Thursday, May 15, 2025

NCC YAJA NA MFUMO KUSAIDIA SEKTA YA UJENZI


Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega akifungua mkutano wa mashauriano na wadau wa sekta ya ujenzi ambayo imefanyika leo jijini Dar es salaam.

Mhandisi Tumaini Lemunge kutoka Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC) akiwasilisha mada  katika mkutano wa mashauriano na wadau wa sekta ya ujenzi ambao umefanyika leo jijini Dar es salaam

.

Baadhi ya washiriki walioshiriki katika mkutano wa mashauriano na wadau wa sekta ya ujenzi ambao imefanyika leo jijini Dar es salaam.

........................

:: Wakandarasi wazembe nao waonywa

Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega, amewataka wakandarasi nchini kutekeleza miradi kwa weledi na kwa kuzingatia viwango, ili kuleta tija kwa taifa.

Akizungumza leo Dar es Salaam wakati akifungua mkutano wa mashauriano na wadau wa sekta ya ujenzi, Mhe. Ulega amesisitiza umuhimu wa wakandarasi kutekeleza kazi zao kwa kuzingatia masharti ya mikataba, maslahi ya wananchi pamoja na taifa kwa ujumla.

Kwa mujibu wake, wakandarasi wana mchango mkubwa katika kuinua uchumi wa nchi. Amesema wanaposhindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo hukwamisha utoaji huduma kwa wananchi, hivyo kusababisha hasara kwa Serikali.

"Tutawachukulia hatua za kisheria wakandarasi wazembe wanaokiuka makubaliano ya mikataba. Serikali ipo pamoja nanyi kwa kuhakikisha kunakuwa na mazingira bora ya kazi, lakini hatutasita kuwawajibisha ikiwa mtakwenda kinuume na makubaliano," Mh Ulega amesema.

Wakati huo huo, Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC) limebuni mfumo mpya wa uchakataji viwango vya bei za ujenzi na matengenezo ya barabara, lengo likiwa kuisaidia sekta ya ujenzi kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Akiwasilisha mfumo wa uchakataji wa viwango vya bei za ujenzi na matengenezo ya barabara katika mkutano huo, Mhandisi Tumaini Lemunge wa NCC, amesema mfumo huo umetengenezwa kwa ushirikiano na wadau mbalimbali wa sekta ya ujenzi.

Mhandisi Lemunge amesema mfumo huo utaaidia taasisi, wahandisi washauri, na wakandarasi kufanya makadirio sahihi ya gharama.

“Mfumo huu utawasaidia watumiaji kuandaa makadirio ya gharama kwa miradi mbalimbali ya ujenzi na matengenezo ya barabara, pia utasaidia kulinganisha bei ya mzabuni na bei halisi ya soko, ili kuhakikisha utekelezaji wa mradi unakuwa na tija,” amesema.

Ameongeza kuwa mfumo huo utapunguza changamoto ya utoaji wa bei zisizoendana na uhalisia wa gharama za miradi, jambo ambalo limekuwa likikwamisha utekelezaji bora wa miradi ya ujenzi.

“Natoa wito kwa wakandarasi wote kuwasiliana na NCC ili waanze kutumia mfumo huu kwa ajili ya kupata bei halisi za zabuni, jambo ambalo litawasaidia kupanga kazi kwa ufanisi,” amesisitiza.

  

RC KATAVI ARIDHISHWA NA MAENDELEO YA MRADI WA UMEME TABORA - KATAVI

Mkurugenzi wa Miradi Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Mhandisi Frank Mashalo (Pili kulia) akitoa ufafanuzi kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe. Mwanamvua Mrindoko, kuhusu maendeleo ya Mradi wa Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovolti 132 kutoka Tabora hadi Katavi unaotekelezwa na Kampuni ya ETDCO ambao umefikia asilimia 96, hayo yamejiri katika  ziara ya Mkuu wa Mkoa huo ya kukagua miradi ya maendeleo iliyofanyika Mei 15, 2025, Mkoani Katavi.

Picha za miundombinu  ya Mradi wa Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovolti 132 kutoka Tabora hadi Katavi unaotekelezwa na Kampuni ya ETDCO  Mkoa wa  Tabora  hadi Katavi.

.......

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mhe. Mwanamvua Mrindoko, ameridhishwa na utekelezaji wa Mradi wa Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovolti 132 kutoka Tabora hadi Katavi, unaotekelezwa na Kampuni ya ETDCO, ambao kwa sasa umefikia asilimia 96.

Akizungumza Mei 14, 2025, akiwa katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Mkoa wa Katavi, Mhe. Mrindoko amewataka wananchi wa Mkoa wa Katavi, hususan wa Wilaya ya Mlele, kujitayarisha kupokea umeme kwa kujiimarisha katika shughuli za uzalishaji ili kujiongezea kipato.

Aidha, Mhe. Mrindoko ametoa rai kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kufikiria kuwekeza katika Mkoa wa Katavi, kwani sasa utakuwa na umeme wa uhakika na wa kutosha.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mlele, Alhaji Majid Mwanga, amewataka wananchi kuilinda na kuitunza miundombinu ya umeme inayojengwa na serikali kwa gharama kubwa.

Nao wananchi wa Wilaya ya Mlele wameishukuru serikali kwa kuwaletea umeme wa Gridi ya Taifa, huku wakisema kuwa hatua hiyo itachochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika maeneo yao.

Katika ziara hiyo Mhe. Mrindoko ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Mlele, Alhaji Mwanga, ambapo amekagua ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 132 kutoka Tabora, pamoja na Kituo cha Kupokea, Kupozea na Kusambaza Umeme cha Inyonga, kilichopo Wilaya ya Mlele.

Wednesday, May 14, 2025

‘VIWANGO VYA UJENZI WA SHULE ZA SERIKALI KUREJESHA UBORA’


NCC kuhakikisha vinadhibiti utoro, hasara kwa matengenezo ya kila wakati

SERIKALI kupitia Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC), lililo chini ya Wizara ya Ujenzi, imetekeleza ahadi yake kwa kuhakikisha viwango na viwango msawazo vya ujenzi bora wa majengo ya shule zake za awali, amali na sekondari vinaandaliwa, ili sekta husika ya elimu ivizingatie au kuvitumia pindi inapoandaa miongozo ya ujenzi wa shule, pamoja na ununuzi wa samani kwa ajili ya shule hizo.

NCC imefanya kazi hiyo kwa kushirikiana na wataalamu wa ujenzi, wahusika wa uboreshaji na matengenezo ya mifumo ya umeme, maji na huduma nyingine muhimu kutoka katika wizara na taasisi mbalimbali, kwa kuandaa rasimu, baada ya kupitia miongozo inayotumika sasa, kuichambua na kuangalia changamoto au mapungufu yaliyopo, hususan kwenye eneo la viwango na viwango msawazo vya ujenzi wa shule na aina ya samani zinazotumika.

Kwa mujibu wa Mratibu wa maandalizi ya viwango na viwango msawazo hivyo, Mhandisi Heri Hatibu ambaye pia ni Mkurugenzi wa Utafiti na Maendeleo wa NCC, lengo la kuandaa viwango na viwango msawazo hivyo ni kuweka muongozo wa usanifu, ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya shule za Serikali.

“Tunafanya hivyo ili kuhakikisha kunakuwa na viwango na viwango msawazo vya ujenzi wa majengo ya shule vinavyoendana na wakati uliopo wa sayansi na teknolojia, vyenye kuzingatia mahitaji halisi ya watumiaji wa majengo, wakiwemo wenye mahitaji maalum, na vyenye kuzingatia usalama wa wanafunzi, walimu na mazingira” Mha. Hatibu amesema.

Aidha, ameongeza kuwa, viwango hivyo vinavyotarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2025/2026, vitasaidia kuongeza ufanisi katika matumizi ya rasilimali za nchi, yatakayowezesha kupangwa bajeti za usimamizi wa miradi ya ujenzi, kwa urahisi.

Wakati akifungua kikao kazi cha kuandaa viwango hivyo mjini Morogoro hivi karibuni, Mtendaji Mkuu wa NCC, Mha. Dkt Matiko Mturi amesema, inapaswa viandaliwe viwango na viwango msawazo vitakavyo rejesha ujenzi wa majengo mbalimbali yakiwemo ya shule, kwenye ubora unaotakiwa, unaozingatia usalama na kuendana na thamani halisi ya gharama zinazotumika, kama ilivyokuwa zamani.

Dkt Matiko anasema, ukiangalia majengo yaliyojengwa miaka mingi iliyopita utagundua kuwa ni bora na hayahitaji matengenezo ya mara kwa mara kama yanayojengwa sasa. Amesema ujenzi wa majengo hayo ulizingatia mambo mengi muhimu ambayo miongozo yetu mingi ya sasa haiyaainishi.

“Ukiangalia maabara za shule zilizojengwa zamani utagundua kuwa za sasa zina walakini. Lakini, si maabara tu, bali hata majengo ya shule za zamani za Serikali ni imara. Kwa sababu hiyo, ninasisitiza muandae viwango na viwango msawazo vitakavyosaidia kuandaliwa kwa miongozo ya ujenzi wa shule hizo, itakayo ondoa mapungufu hayo,” amesema.

Mha. Ronald Mwajeka wa Idara ya Maendeleo ya Miundombinu katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ametaja baadhi ya mapungufu yaliyopo katika viwango na viwango msawazo vilivyopo kwenye miongozo inayotumika katika ujenzi wa shule za serikali, ambayo yamepatiwa ufumbuzi kuwa ni

Maeneo yaliyokuwa na changamoto na kupatiwa suluhisho kwa kuwekewa viwango ni pamoja na uchaguzi wa eneo/maeneo ya ujenzi, vigezo stahiki vya kuzingatia katika kutekeleza ujenzi, vielelezo vya kuzingatia wakati wa usimamizi na ukaguzi wa kazi za ujenzi. Mengine ni eneo la ubora na uimara wa vifaa vinavyotumika katika ujenzi, kuwekwa kwa viwango vya chini vitakavyozingatiwa wakati wa ujenzi, kuhakikisha kuwa jengo linaweza kutumika na watu wa hali zote. Amesema awali viwango havikugusia shule za amali lakini vya sasa vimezizingatia.

Mtaalamu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Bi. Agricia Mtakyawa amesema viwango na viwango msawazo vinavyo andaliwa vitapunguza matumizi ya fedha za Serikali kwenye huduma za maji, umeme na nyingine, kwa sababu vimeelekeza ujenzi utakaoruhusu uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua, pamoja na matumizi zaidi ya nishati ya umeme wa jua.

“Majengo ya shule yatazingatia ukubwa wa madirisha unaoruhusu hewa na mwanga wa kutosha, taa za umeme zinazotumia ‘sensor’ ambapo panapokuwa na mtu darasani zinawaka zenyewe na kujizima pindi wanafunzi na walimu wote wanapotoka darasani, au bwenini, ofisini kwa wanaohusika na maeneo hayo.   

Monday, May 12, 2025

INEC YAGAWA MAJIMBO YAANZISHA CHAMAZI NA KIVULE DAR

........................

TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imeanzisha majimbo mapya nane nchini kote, ambapo jijini Dar es Salaam, majimbo mawili ya Chamazi na Kivule yameanzishwa kutokana na mgawanyo wa majimbo ya Mbagala wilayani Temeke na Ukonga Wilaya ya Ilala.

Majimbo mapya yatakuwa sehemu ya Uchaguzi Mkuu wa Rais na Wabunge, unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu, ambapo Mwenyekiti wa INEC, Jaji wa Rufani Jacob Mwambegele, amesema tume yake imefikia uamuzi huo baada ya kupitia maombi kutoka kwenye mikoa mbalimbali nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Jaji Mwambegele amesema uamuzi huo umefanyika kwa kuzingatia masharti ya Ibara ya 75(1), (2) na (4) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 ikisomwa pamoja na Kanuni ya 18(7) ya Kanuni za Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi za Mwaka 2024.

Ameyataja majimbo hayo kuwa ni Jimbo la Kivule amabalo limegawanywa kutoka Jimbo la Ukonga na Jimbo la Uchaguzi la Chamazi lililogawanywa kutoka Jimbo la Mbagala yote ya mkoani Dar es Salaam.

“Mkoani Dodoma limeanzishwa jimbo jipya moja, ambapo Jimbo la Uchaguzi la Dodoma Mjini limegawanywa na kuanzishwa jimbo jipya la Uchaguzi la Mtumba na Mkoani Mbeya limeanzishwa jimbo jipya moja, ambapo Jimbo la Uchaguzi la Mbeya Mjini limegawanywa na kuanzishwa Jimbo jipya la Uchaguzi la Uyole,” amesema.

Jaji Mwambegele ameongeza kuwa, Mkoani Simiyu limeanzishwa jimbo jipya moja ambapo Jimbo la Uchaguzi la Bariadi limegawanywa na kuanzishwa Jimbo jipya la uchaguzi la Bariadi Mjini.

“Huko Geita yameanzishwa majimbo mawili, Jimbo la Busanda limegawanywa na kuanzishwa Jimbo jipya la Katoro na Jimbo la Chato likigawanywa pia na kuanzishwa Jimbo jipya la Chato Kusini.

“Mkoani Shinyanga limeanzishwa jimbo jipya moja, ambapo Jimbo la Uchaguzi la Solwa limegawanywa na kuanzishwa Jimbo jipya la Uchaguzi la Itwangi,” amesema Jaji Mwambegele mbele ya wanahabari.

Sunday, May 11, 2025

NYAHOZA AKIPONGEZA CHAMA CHA CCK KWA KUMPATA MGOMBEA URAIS

Naibu Msajili wa vyama vya siasa nchini Sisty Nyahoza akizungumza na wajumbe wa Chama Cha Siasa Cha Kijamii (CCK) katika mkutano Mkuu maalum wa Chama hicho kwa ajili ya kuwachagua na kuwapitisha wagombea nafasi ya Urais wa Tanzania Bara na Zanzibar ambao umefanyika tar 10/5/2025 jijini Dar es salaam.

Mwenyekiti Taifa wa Chama cha Kijamii cha CCK David Daudi Mwaijolele ambaye pia amepitishwa kwa kupigiwa kura kugombea nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bara akizungumza katika mkutano Mkuu maalum wa Chama hicho ambao umefanyika tar 10/5/2025 jijini Dar es salaam.

Aisha Salum Hamadi ambaye amepitishwa kugombea nafasi ya Urais kupitia Chama cha Kijamii cha CCK Zanzibar akizungumza na wajumbe wa chama hicho katika mkutano Mkuu maalum wa Chama hicho ambao umefanyika tar 10/5/2025 jijini Dar es salaam.

Viongozi wa Kitaifa wa Vyama vya siasa waliohudhuria katika katika mkutano Mkuu Maalum wa Chama cha siasa cha Kijamii cha CCK ambao umefanyika tar 10/5/2025 jijini Dar es salaam.

Wajumbe mbalimbali waliohudhuria katika mkutano Mkuu Maalum wa Chama cha siasa cha Kijamii cha CCK ambao umefanyika tar 10/5/2025 jijini Dar es salaam. 

........................

NA MUSSA KHALID

Naibu Msajili wa vyama vya siasa nchini Sisty Nyahoza amekipongeza Chama Cha Siasa Cha Kijamii - CCK kwa kufanya Uchaguzi wa wazi na demokrasia wa kumchagua Mgombea Urais wa Tanzania bara na Zanzibar kupitia Chama hicho.

Katika Uchaguzi huo uliofanyia jijini Dar es salaam wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalum wa Chama hicho wamepiga kura na kumchagua Mwenyekiti wa Chama hicho David Daudi Mwaijojele kuwa mgombea Urais kwa Tanzania Bara huku  Isha Salum akiteuliwa na Halmashauri kuu kuwa mgombea Pekee wa Nafasi ya Urais Kupitia Chama Cha CCK  Zanzibar.

Akizungumza kwenye mkutano huo Naibu Msajili wa vyama vya siasa Sisty Nyahoza amevisisitiza Vyama vya siasa nchini kueendelea kudumisha amani na kulinda umoja wetu wakati huu wa kuelekea uchaguzi ili nchi iweze kupita salama.

Nyahoza amesema mkutano huo umefanyika kwa sababu taifa lina amani na hivyo mtu yeyote mwenye nia ya kuvunja amani ni vyema akakemewa mapema.

‘Umoja wetu ndio unatufanya tuwe Pamoja hapa tukiwa wazanzibari na watu wa bara hivyo tulinde umoja wetu ili tfanye siasa kwa amani na utulivu’amesema Nyahoza

Kwa upande wake Mwenyekiti Taifa wa Chama cha Kijamii cha CCK David Daudi Mwaijolele amesema kuwa wananchi watarajie makubwa pindi atakapofanikiwa kuitangaza mikakati mbalimbali wakati wa kampeni.

Amesema kuwa malengo yao ni kutaka kuhakikisha jamii ya kitanzania inaishi maisha bora katika maeneo mbalimbali ya kilimo ,uvuvi,ujasiriamali ikiwemo makundi maalum.

‘Chama cha CCK tutakapopewa ridhaa kupitia tume Tutahakikisha vijana wanaweza kujiajiri wenyewe pindi wanapomaliza elimu,lakini pia wanawake kunufaika na uchumi wao’amesema Mwaijolele

Naye Aisha Salum Hamadi ambaye amepitishwa kugombea nafasi ya Urais kupitia chama chake cha CCK Zanzibar amesema kuwa anajivunia kuwa mwanamke wa kwanza chama chake kumuamini kuiepeperusha bendera ya chama katika visiwa hivyo.

Amesema kuwa yupo tayari kukipambania chama cha CCK kwa Zanzibar ambapo vipaumbele vyake ni kuwasaidia watui wenye uhitaji wakiwemo walemavu.

Amewasisitiza watanzania kuwaonyesha mshikamano kwa kuwaunga mkono kukichagua chama chao ili kiweze kuwasaidi kuzitatua changamoto mbalimbali kwenye maeneo yao.

   

Friday, May 9, 2025

KAPINGA AZINDUA KITUO MAMA CHA GESI ASILIA ILIYOSHINDILIWA (CNG) JIJINI DAR ES SALAAM

.............................

Ni cha Pili kwa ukubwa barani Afrika; Cha Kwanza kwa ukubwa EAC

 Kujaza Gesi Asilia kwenye magari 1200 kwa siku

 Ampongeza Dkt. Samia kutatua changamoto za wananchi kwa vitendo

Aipongeza TPDC; Ataka Vituo vya CNG kuendelea kujengwa

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga amezindua Kituo Mama cha Gesi Asilia iliyoshindiliwa (CNG) ambacho kina uwezo wa kujaza Gesi Asilia kwenye magari 1200 kwa siku huku kikifanya kazi kwa muda wa saa 24. 

Kapinga amezindua kituo hicho tarehe 9 Mei, 2025 jijini Dar es Salaam akimwakilisha Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ambapo uzinduzi huo ulienda sambamba na uzinduzi wa basi la mfano la Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART) ambalo litaendeshwa kwa kutumia nishati ya Gesi Asilia.

Akizungumza na halaiki iliyohudhuria hafla hiyo, Kapinga amemshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono, mtazamo na maelekezo yake kwa Wizara ya Nishati ambayo yanaleta matokeo chanya kielelezo mojawapo kikiwa ni uzinduzi kwa kituo hicho cha CNG.

Pia, amemshukuru Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko kwa uongozi wake ambao unapelekea upatikanaji wa nishati ya uhakika ambayo ni rafiki kwa mazingira na afya za wananchi.

“ Hapo nyuma kumekuwa na malalamiko ya uwepo wa foleni kubwa za ujazaji wa gesi kwenye vyombo vya moto katika vituo vya CNG ikiwemo kituo cha Ubungo Maziwa, lakini uwepo wa kituo hiki unaonyesha jinsi Serikali inavyotekeleza kwa vitendo ahadi inazotoa kwa wananchi za kupunguza kero ya upatikanaji wa CNG, nampongeza Rais Samia kwa kuendelea kutatua changamoto za wananchi na pia naipongeza Bodi na Menejimenti ya TPDC kwa hatua hii.” Amesema Kapinga

Ameeleza kuwa, kituo hicho kitakuwa na uwezo wa kujaza Gesi kwenye magari nane kwa wakati mmoja, kuchochea ongezeko la vituo vingine vya CNG na kuwapatia huduma ya gesi watumiaji wengine kama viwanda, shule, hoteli n.k

Kapinga ameiagiza TPDC kuhakikisha kuwa, kituo hicho kinakuwa mfano wa kutoa huduma bora na za viwango kwa wateja huku kikizingatia masuala ya usalama na utunzaji wa mazingira.

Pia ameiagiza TPDC kuendelea kujenga vituo vya CNG katika maeneo mengine ya nchi ikiwemo Lindi na Mtwara, pia kutoa ushirikiano kwa sekta binafsi ili kuendelea kuchochea uwekezaji kwenye sekta ya CNG. 

Naibu Waziri Kapinga pia ameishukuru Sekta binafsi kwa kuendelea kuiunga mkono Serikali kwenye ujenzi wa vituo vya CNG.

Aidha, amewaasa Watanzania kuchangamkia fursa ya kuweka mifumo ya matumizi ya gesi kwenye magari yao kwani mifumo hiyo haiharibu magari hayo na pia watapata nafuu ya gharama za uendeshaji. 

Kuhusu kampuni ya UDART ambayo kwa mara ya kwanza imezindua basi jipya linalotumia Gesi Asilia, ikiwa ni moja ya mabasi mengi yakayotumia gesi hiyo, Kapinga amesema kuwa ushirikiano kati ya TPDC na UDART utaendelea kuchochea uwekezaji kwenye CNG na kuendelea kuboresha huduma za usafiri jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Albert Msando akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, ameipongeza wizara ya Nishati kwa kazi kubwa inayofanyika ili kupata matokeo makubwa kwenye sekta na kuahidi ulinzi katika miundombinu hiyo ambayo ni muhimu katika kutoa huduma kwa wananchi.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe.Kilumbe Ng’enda amesema Bunge limeridhishwa na hatua zinazochukuliwa kwa kasi na Serikali katika kuendeleza Sekta ya Gesi akieleza kuwa unapotumia gesi asilia kuendesha gari unapata unafuu kwa asilimia 40 ukilinganisha na mafuta. 

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio ameipongeza Bodi na Menejimenti ya TPDC kwa kutekeleza mradi huo kwa mafanikio, pia ameipongeza UDART ambao watakuwa wateja wakubwa wa CNG.

Amesema mradi huo ni wa kujivunia kwani kituo hicho kilichozinduliwa ni cha Pili kwa ukubwa barani Afrika na cha kwanza kwa ukubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki

Mwenyekiti Bodi TPDC, Mhe. Balozi Ombeni Sefue amesema Bodi na Menejimenti ya Taasisi hiyo itahakikisha changamoto ya wananchi kupanga foleni ndefu kwenye vituo vya CNG inaisha na watahakikisha rasilimali ya gesi asilia inapatikana wakati wote kupitia huduma mbalimbali ikiwemo ya kupikia na kuendeshea vyombo vya moto.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Francis Mwakapalila amesema kuwa katika kuchochea matumizi ya Gesi Asilia kwenye vyombo vya moto nchini, TPDC imeamua kuweka mkazo kwa kuwekeza katika ujenzi wa vituo vya kujazia gesi asilia kwenye vyombo vya moto ikiwemo magari na bajaji kwenye maeneo mbalimbali nchini na kwa sasa tayari wameanza mchakato wa manunuzi ya vituo vitano vya CNG vinavyohamishika ambavyo vitawejwa kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Dodoma.

Awali Mkurugenzi wa Idara ya Biashara ya Mafuta kutoka TPDC, Mhandisi Emmanuel Gilbert alisema kuwa kituo hicho kina uwezo wa kuzalisha CNG kiasi cha futi za ujazo milioni 4.2 sawa na kilo 120 kwa siku, kina pampu nne zenye jumla ya nozeli nane na hivyo kukifanya kituo kuwa na uwezo wa kuhudumia magari nane kwa wakati mmoja ambapo kwa siku kitatoa huduma kwa magari takriban 1200.

Ameongeza kuwa, kituo kina pampu maalum tatu kwa ajili ya kujaza magari maalum ya kusafirisha CNG kwenda kwenye vituo vidogo vya kujaza gesi kwenye magari (Offline CNG Filling Stations), viwandani, taasisi na majumbani.  

WAZIRI MKUU AONGOZA KIKAO CHA KAMATI YA KITAIFA YA MAZISHI YA VIONGOZI

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo Mei 09, 2025 ameongoza Kikao cha Kamati ya Kitaifa ya Mazishi ya aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Hayati Cleopa David Msuya kilichofanyika katika Ofisi ya ndogo za Waziri Mkuu, Magogoni Jijini Dar es Salaam.

TANZANIA YAWAKILISHWA VEMA KWENYE KAMBI YA MAFUNZO YA HUWAWEI

 

Wanafunzi wenye vipaji katika sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano kutoka vyuo vikuu 12 duniani, wameshiriki katika kambi ya mafunzo ya kimataifa ya Huawei Global Seeds for the Future, iliyofanyika kuanzia Aprili 9 hadi Aprili 17, 2025 katika makao makuu ya Huawei huko Shenzhen nchini China. 

Kambi hiyo ya mafunzo ilibeba maudhui yenye lengo la kuwaongezea uwezo wanafunzi hao katika maeneo mbalimbali ikiwa ni pamoja na eneo la kidigiti, ubunifu na ujasiriamali. 

Kambi hiyo iliyodumu kwa muda wa wiki moja ni sehemu ya mkakati wa kampuni hiyo ya teknolojia ya mawasiliano ya Huawei katika kuendelea kuwawezesha vijana wenye vipaji katika sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano. 

Nchi zilizoshiriki kambi hiyo ya mafunzo nchini China ni pamoja na Tanzania, Algeria, Cambodia, Laos, Uturuki, Ireland, Brazil, Mexico, Azerbaijan, Pakistan, Ethiopia na Afrika Kusini. 

Akizungumzia mkakati huo wa Huawei, mmoja wa wanufaika kutoka Tanzania akiiwakilisha Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam (DIT) ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa nne wa Shahada ya kwanza ya Sayansi katika Uhandisi wa Kielektroniki na Mawasiliano, Natasha Nassoro amesema mada za mwaka huu hazikuacha mshiriki yeyote nyuma akiweka bayana kuwa walijifunza mambo ya ndani na nje ya tasnia ya Tehama (ICT ) chini ya mpango ulioandaliwa vyema, ukihusisha utafiti na kupendekeza teknolojia tofauti za kuchagiza juhudi za uendelevu duniani chini ya mpango wa tech4good pamoja na kujenga na kuunganishwa na mtandao wa mabingwa wengine wenye vipaji. 

Ujumbe wa wanafunzi hao kutoka vyuo 12 duniani pia ulipata fursa ya kufanya ziara katika vituo vya maendeleo ya kiteknolojia kama vile kampuni ya Alibaba, kituo cha mafunzo cha Huawei Global, Red note, duka la Huawei Flagship pamoja na ziara za kitamaduni huko Shanghai, kutembelea mgahawa maarufu duniani na ziara ya ya kutembelea Jiji la Shenzhen.

Huawei ilizindua programu ya Seeds For the Future nchini Thailand mwaka 2008, na hadi kufikia mwaka huu imefanikiwa kuwakusanya pamoja wanafunzi kutoka nchi 141 duniani huku zaidi ya wanafunzi 18,000 wakinufaika. 

Seeds for the Future ni programu kuu ya Huawei ya kurudisha kwa jamii (CSR), na imekuwa ikiendeshwa kwa kuchagua vipaji vya vijana kutoka duniani kote ili kushiriki katika mafunzo ya muda mfupi yanayolenga kuwashindanisha kwenye teknolojia, kubadilishana tamaduni na kukuza moyo wa ujasiriamali. 

Mpango huo umekuwa pia ukitoa nafasi ya upendeleo kwa wanawake kwa kiwango cha ushiriki cha angalau theluthi moja wawe wanafunzi wa kike.