JSON Variables

Header Ads Widget

Responsive Advertisement
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Top Stories. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Top Stories. Onyesha machapisho yote

Ijumaa, 13 Juni 2025

KAMPENI YA PIKA SMART INAYOHAMASISHA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA YAZINDULIWA


.........................

Kamishna Luoga asisitiza matumizi ya umeme katika Nishati Safi ya Kupikia

Kamishina wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amezindua kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ya umeme inayokwenda na kaulimbiu ya PIKA SMART.

Mha. Luoga amezindua kampeni hiyo leo Juni 13, 2025 jijini Dar es Salaam akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba. 

Kampeni hiyo imeandaliwa na Shirika la Modern Energy Cooking Services (MECS) chini ya ufadhili wa UKAID kwa kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Nishati.

Mhandisi Luoga amesema kampeni hiyo imezinduliwa ikiwa ni mojawapo ya jitihada za Serikali kuhakikisha inawahamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia ili kufikia lengo la asilimia 80 ya watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034. 

Luoga amewatoa hofu wananchi kuhusu kutumia nishati safi ya kupikia ya umeme akitanabaisha kuwa ni salama na gharama nafuu na kuongeza kuwa Tanzania Ina Umeme mwingi na wa kutosheleza mahitaji.

"Kama tunavyofahamu bwawa la kufua umeme kwa maji la Julius Nyerere limekamilika na hivyo kupelekea umeme uliopo nchini hadi sasa kufikia takribani megawati 4,031, umeme huu umeshafika katika Vijiji vyote 12, 318 vya Tanzania hivyo kuna kila sababu kwa wananchi kutumia nishati safi ya umeme kupikia." amesema Mha. Luoga

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Mkurugenzi wa Mipango na uwekezaji TANESCO, Mhandisi Henryfried Byabato amesema Shirika hilo limekuwa likihamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia ya umeme kutokana na uwepo wa kutosha wa nishati hiyo nchini.

Ameongeza kuwa, teknolojia zimeboreshwa hivyo majiko ya umeme yanatumia nishati kidogo na kwa ufanisi mkubwa.

Kampeni hii ya kuhamasisha matumizi ya pika smart imekuja wakati muafaka ambapo Wizara ya Nishati imezindua mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wenye lengo la kutoa mwongozo kwa wadau kuendeleza kampeni ya uhamasishaji matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati safi ya kupikia kuhakikisha watanzania wanahama kutoka kwenye matumizi ya nishati isiyo safi kwenda kwenye nishati safi

Alhamisi, 12 Juni 2025

CP. WAKULYAMBA AWATAKA MAOFISA WA NCAA KUWA WAADILIFU.


*********

Na Sixmund Begashe,Karatu

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Uhifadhi, Kamishna wa Polisi (CP) Benedict Wakulyamba, amewavisha vyeo Maofisa 22 na Askari watatu wa Jeshi la Uhifadhi la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) waliokamilisha mafunzo ya mabadiliko kutoka mfumo wa kiraia kwenda kijeshi.

Akizungumza katika hafla iliyofanyika Kituo cha Mafunzo Mbulumbulu mkoani Arusha, CP Wakulyamba amewataka wahitimu hao kuyaishi kwa vitendo mafunzo hayo kwa kufuata nidhamu ya kijeshi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Amesisitiza kuwa Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ina imani kubwa na Jeshi la Uhifadhi katika kulinda rasilimali za Taifa, hivyo ni lazima kila mmoja afanye kazi kwa bidii, uadilifu na kuepuka vitendo vya rushwa.

Ameonya kuwa hatua kali za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayehusika na vitendo vya uhalifu au kushindwa kusimamia maadili ya jeshi.

Aidha, CP Wakulyamba amepongeza wahitimu kwa ubunifu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia katika kituo hicho, akisema ni utekelezaji wa agizo la Rais kuhusu kupunguza matumizi ya kuni na mkaa na kuhimiza taasisi nyingine za Wizara kuiga mfano huo.

Jumatano, 11 Juni 2025

USAWA WA KIJINSIA NI KIPAUMBELE CHA SERIKALI- DKT. JINGU


...........................

Na WMJJWM, Dodoma.

Katibu Mkuu wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. John Jingu amesema Serikali inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imezingatia masuala ya Usawa wa kijinsia katika nyanja mbalimbali ikiwa juhudi za Serikali katika kuleta Usawa huo katika jamii.

Dkt. Jingu ameyasema hayo Juni 11, 2025 jijini Dodoma alipokutana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya Usawa wa Jinsia (UN Women), Hodan Addou kwa ajili ya kujadili utekelezaji wa afua mbalimbali nchini juu ya uwezeshaji wanawake kiuchumi.

Dkt. Jingu ameeleza kwamba Serikali inaendelea na juhudi mbalimbali kuhakikisha kwamba  Jamii inaamka na kuachana na ukatili wa kijinsia ambao umekua ni kikwazo cha maendeleo kwa ujumla.

“Kuna Kampeni ya Amsha Ari  inayoendelea ambayo imelenga kujenga ufahamu juu ya masuala mbambali ya kimaendeleo kwa wananchi katika mikoa yote  nchini ikiwemo suala zima la kuwainua wanawake kiuchumi“ amesema Dkt. Jingu.

Aidha Dkt. Jingu amelipongeza Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na ustawi wa Jinsia (UN Women) kwa kazi nzuri linalofanya katika kuunga mkono juhudi za Serikali ili kuleta usawa wa jinsia nchini na kuwaeleza kuwa wanaweza kuongeza nguvu katika kampeni hiyo ya mageuzi ya kifikra ya “Amsha Ari” ili kuweza kukuza usawa wa kijinsia nchini.

Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya Usawa wa Jinsia (UN Women) Hodan Addou ameahidi kuwa Shirika hilo litaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupunguza na ukatili wa kijinsia na kukuza usawa wa kijinsia.

MWISHO.

SERIKALI YAMUONYA ALIYESAMBAZA UZUSHI WENYE VIDOTI MIGUUNI WANA VVU


......................
Serikali imeonya watu wote wasio na utalaam kujiepusha kutoa taarifa za afya huku wakijua hawana weledi au taaluma ya kufanya hivyo.

Imesema hatua kali za Sheria zitachukuliwa dhidi ya mtu yoyote atakayetoa na kusambaza taarifa zinazopotosha jamii na kufifisha juhudi za Serikali na wadau katika kupambana na maambukizi ya Virusi Vinavyosababisha Ugonjwa wa Ukimwi (VVU).

Taarifa ya Wizara ya Afya iliyosainiwa na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali, Roida Andusamile ilisema imeona taarifa ya video inayosambaa katika mitandao ya kijamii wa Instagram inayoonyesha mtu anayejitambulisha kuwa anaishi na virusi vya Ukimwi kwa jina la Mentor Chery and wellbeinghub akitoa taarifa kuwa dalili mojawapo ya kuwa na virusi hivyo ni mtu kuwa na vidoti vyeusi katika dole gumba la mguu hadi kisigino.

"Mtu huyo ameenda mbali zaidi na kuiasa jamii hasa walio katika uhusiano wachunguze wenzi wao wasiojua hali zao za maambukizi ya Virusi hivyo na endapo watabaini hayo ni wazi kuwa wenzi hao wameathirika kwa kuwa wenye ugonjwa huo nyao.zao haziwi nyeupe," ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

Kwa mujibu wa Wizara ya Afya, taarifa hiyo inapotosha jamii. Ukweli ni kwamba huwezi kumtambua muathiriia wa Virusi vinavyosababisha Ukimwi kwa kumuangalia kwa macho au kwa kuangalia baadhi ya dalili zilizoelezwa katika video hiyo. Badala yake njia pekee ya kumtambua hali ya anayeishi na virusi hivyo ni kwa kufanya vipimo kwa mujibu wa miongozo iliyopo

Jumanne, 10 Juni 2025

CP. WAKULYAMBA:SIMAMIE MAJUKUMU YA UHIFADHI, MSIJIHUSISHE NA RUSHWA

............….

Na Sixmund Begashe, Katavi

Maofisa na Askari wapya wa Jeshi la Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) wametakiwa kusimamia ipasavyo majukumu ya uhifadhi katika maeneo watakayopangiwa ili kuimarisha ulinzi wa rasilimali za taifa na kujiepusha na vitendo vya rushwa.

Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Kamishna wa Polisi Benedict Wakulyamba alipokuwa akifunga mafunzo ya Maofisa na Askari hao 238 katika Kituo cha Mafunzo Mlele, mkoani Katavi.

CP. Wakulyamba amesisitiza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kulinda mazingira na rasilimali za taifa na kuwasihi kujenga mshikamano, nidhamu na maadili mema katika utendaji wao wa kazi.

"Hakikisheni mnakuwa waadilifu, watiifu na wanyenyekevu katika utekelezaji wa amri halali kutoka kwa viongozi wenu na kamwe msijihusishe na vitendo vya rushwa,"amesema.

Ameongeza kuwa "Jeshi la Uhifadhi halitavumilia askari au Ofisa yeyote atakayehujumu juhudi za uhifadhi kwa kupokea rushwa au kuruhusu shughuli haramu kama uingizaji wa mifugo na uchimbaji wa madini ndani ya hifadhi."

Naibu Katibu Mkuu huyo amewapongeza Askari na Maofisa wote waliomaliza mafunzo hayo kwa mafanikio na kuwashukuru wakufunzi waliojitolea kuhakikisha mafunzo ya miezi sita yanafanikishwa kwa ubora unaotakiwa.

Mafunzo hayo ni sehemu ya maboresho ya utendaji katika Jeshi la Uhifadhi la TANAPA na wahitimu 238 waliohitimu kati yao, 229 ni Askari waliopitia kozi ya awali ya Jeshi la Uhifadhi, watatu wamehitimu kozi ya mabadiliko ya muundo wa utendaji kazi na sita wamehitimu kozi ya Uongozi kwa Askari Uhifadhi waliopandishwa vyeo kuwa Maofisa.


NIRC YAENDELEA NA UTELEKELZAJI WA AHADI YA RAIS SAMIA KUCHIMBA VISIMA 67,000 VYA UMWAGILIAJI,NCHI NZIMA

  NIRC; Dodoma 

 Serikali ya Awamu ya Sita, kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, imeanza utekelezaji wa ahadi ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya uchimbaji wa visima virefu 67,000 vya maji kwa ajili ya kiliko cha Umwagiliaji nchini.

Lengo ni kuhakikisha kuwa Taifa linaondokana na kilimo cha kutegemea mvua na kuwa na uhakika wa maji kwa ajili ya kilimo na kulima zaidi ya mara moja kwa mwaka

Hatua hiyo imetokana na ahadi ya Rais Dkt.Samia, aliyoitoa wakati wa maazimisho ya siku ya Wakulima Duniani( Nane Nane), yaliyofanyika kitaifa jijini Mbeya, mwaka 2023.

Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma na Mkurugenzi Mkuu Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC), Bwana Raymond Mndolwa, wakati wa kuanza kwa zoezi la uchimbaji wa visima kwa kutumia mitambo iliyonunuliwa na Serikali katika mashamba ya BBT (Chinangali) ya programu ya *Jenga Kesho iliyo Bora* (BBT), inayowawezesha vijana kujiajiri katika kilimo.

Mndolwa amesema Serikali ya Dr. Samia imeiwezesha Tume kununua mitambo ya kisasa ya kuchimba visima virefu, lengo likiwa ni kuhakikisha kunakuwa na mazingira wezeshi ya upatikanaji wa maji kwa ajili ya kiliimo cha Umwagiliaji na Taifa linaondokana na kilimo cha msimu mmoja na kulima mara mbili au zaidi.

“Tume imenunua mitambo 17 ya kuchimba visima kwa thamani ya shilingi bilioni 17.5 yenye uwezo wa kuchimba mita 300 hadi 1,800, ambapo mitambo 7 inachimba visima katika shamba hili la Chinangali na tunashuhudia visima vikiwa na maji ya kutosha kabisa.

“Miundombinu yote ya Umwagiliaji katika shamba hili ipo tayari na sasa hatua inayofuata ni kuhakikisha maji yanapatikana kwa kuchimba visima 29 hapa na visima vingine 40 vitachimbwa katika shamba la BBT (Ndogowe) ili vijana waliopata mashamba haya walime kwa uhakika. Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kwa nguvu mpya, imejidhatiti kutimiza jukumu hilo muhimu”, amesema.

Mndolwa amesema, dhamira hiyo haishii Chinangali na Ndogowe pekee na kwamba Mpango wa uchimbaji visima unatarajiwa kutekelezwa nchi nzima na kuhakikisha kuwa siyo vijana tu, bali wakulima wa kada zote wanapata maji ya uhakika kwa kilimo endelevu.

"Mitambo hii itapita mkoa kwa mkoa, wakulima wajiandae kuchangamkia fursa hii wakiwa katika makundi ya wakulima zaidi ya 16 na ekari kuanzia 40 ili waweze kupata kisima"

Mndolwa ameongeza kuwa Serikali ya Dr. Samia imedhamiria kwa dhati kubwa kumwinua mkulima wa Tanzania ambapo miaka minne iliyopita, miradi ya umwagiliaji ilikuwa 13 pekee, lakini leo hii idadi imeongezeka hadi kufikia miradi 780 pamoja na mpango huu wa visima 67,000 nchi nzima. 

NAIBU WAZIRI KHAMIS ATAKA FUKWE KUTOCHAFULIWA


............................

Naibu wa Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amewataka wananchi wanaofanya shughuli kwenye fukwe kutoharibu mazingira na badala yake wafuate sheria ikiwemo kutotupa taka ovyo.

Ametoa wito huo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Mhe. Asya Mwadini Mohammed aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kusimamia utunzaji wa mazingira ya fukwe. 

Akiendelea kujibu swali hilo, Naibu Waziri Khamis amesema kuwa Serikali inaendelea kuchkua hatua za kusimamia sheria ambayo inawataka wananchi kuacha kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita 6o kando mwa vyanzo vya maji. 

”Ni kweli kuna baadhi ya shughuli zinafanyika kwenye kingo za bahari, kingo za mito na hata kingo za mawiwa ambayo ni vyanzo vya maji vinavyosaidia shughuli za kiuchumi na sasa zipo hatua ambazo Serikali tumezichukua ikiwemo usimamizi wa sheria na kutoa elimu,” alisema. 

Aidha, Mhe. Khamis alisema Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana Mamlaka ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA) itaendelea kupambana na vitendo vya uharibifu wa mazingira katika Mlima Kilimanjaro vikiwemo uchomaji wa moto. 

Alisema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Shally Raymond aliyetaka kufahamu Serikali ina moango gani wa kuhakikisha theluji ya Mlima Kilimanjaro ambayo ni kivutio cha utalii haiyeyuki.

Mhe. Khamis alisema Serikali itaendelea kutumia sheria, miongozo, kanuni na kampeni ambazo zina maelekezo ya mbalimbali ya utunzaji wa vyanzo uvya maji, upandaji miti, kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia. 

Awali, akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalumu Mhe. Esther Malleko lililoulizwa kwa niaba yake na Mhe. Shally kuhusu Serikali ina mpango gani wa kudhibiti uharibifu wa mazingira unaotokana na shughuli za kibinadamu, Mhe. Khamis alisema uharibifu wa mazingira unaotokana na shughuli za kibinadamu unatokea katika sekta nyingi nchini.

Hivyo, alisema ili kudhibiti uharibifu huo, Serikali imechukua hatua mbalimbali ikiwemo kuandaa Sera, Sheria kanuni mikakati na miongozo mbalimbali inayobainisha hatua zinazochukuliwa kukabiliana na changamoto hizo.

Alitaja Sera ya Taifa ya Uhifadhi wa Mazingira ya 2021, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Sura 191 ikisomwa pamoja na marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira Na.5/2025 na Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2032) ni hatua zilizochukuliwa.    

Naibu Waziri Khamis aliongeza kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu uhifadhi wa mazingira na changamoto za mabadiliko ya tabianchi kwa njia mbalimbali, ikiwa ni pamoja na vyombo vya habari, ziara za viongozi na mafunzo mashuleni


Jumatatu, 9 Juni 2025

CP. WAKULYAMBA AWAPA SOMO ASKARI WA JU.

...............

Na Sixmund Begashe, Katavi

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia masuala ya Uhifadhi, Kamishna wa Polisi (CP) Benedict Wakulyamba, ametoa semina elekezi kwa Maofisa na Askari Wanafunzi wa Kozi ya 11 ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), katika Kituo cha Mafunzo ya Kijeshi cha Mlele, mkoani Katavi.

Katika semina hiyo, CP Wakulyamba amesisitiza masuala muhimu yanayohusu utendaji kazi wenye weledi, mahusiano bora kazini, madhara ya utendaji mbovu, pamoja na kazi za msingi za uhifadhi wa maliasili.

Aidha, amewahimiza Maofisa na Askari hao kujiepusha na vitendo vya rushwa na maadili mabovu kazini, huku akiwataka wajikite kujifunza na kuelewa vyema sheria husika, hasa zile zinazohusu uhifadhi wa maliasili.

“Ni lazima mjiepushe na utendaji mbovu. jiepusheni na rushwa, mjenge mahusiano mema na wananchi. Mkitaka kufanikisha majukumu yenu, mshirikiane kwa karibu na wananchi hao,” amesisitiza CP Wakulyamba.

Semina hiyo ni sehemu ya maandalizi kuelekea kufungwa kwa mafunzo rasmi ya Maofisa na Askari 229 wa Jeshi la Uhifadhi (JU) kutoka TANAPA kesho Juni 10, 2025 katika kituo hicho cha Mlele.

 

UKATILI DHIDI YA WATOTO NA VIJANA WAPUNGUA: WAZIRI DKT. GWAJIMA


....................
Na WMJJWM-Dar Es Salaam 

📌 Serikali yaahidi kutumia matokeo hayo kupanga mikakati na mipango na programu mbalimbali ya Serikali za kupambana na Ukatili.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amesema matokeo ya Utafiti wa Ukatili dhidi ya Watoto na Vijana wa mwaka 2024 yanaonesha Ukatili umepungua ukilinganisha na Utafiti kama huo uliofanywa Mwaka 2009.

Dkt. Gwajima ameyasema hayo wakati akitangaza matokeo ya utafiti huo Juni 9, 2025 Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Gwajima amesema, utafiti huo unaonesha kupungua kwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto wa kike ambapo, ukatili wa kingono umepungua kutoka asilimia 33 hadi asilimia 11,  Ukatili wa kimwili umepungua kutoka asilimia 76 hadi asilimia 24 na Ukatili wa kihisia umepungua kutoka asilimia 25 hadi asilimia 22.

Aidha, kwa watoto wa kiume, Ukatili wa kingono umepungua kutoka asilimia 21 hadi asilimia 5, Ukatili wa kimwili umepungua kutoka asilimia 74 hadi asilimia 21 na Ukatili wa kihisia umepungua kutoka asilimia 31 hadi asilimia 16.

"Naomba mfahamu kuwa, huu ni utafiti wa Pili wa kitaifa ambao umefanyika baada ya miaka 15 tangu utafiti ule wa kwanza wa mwaka 2009. Matokeo ya utafiti yanaonesha ukatili umeshuka kwa kiwango kikubwa ukilinganisha utafiti wa 2009 na huu wa 2024" amesema Dkt. Gwajima

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum itafanya tathmini, mapitio na maboresho ya Sera na Sheria zilizopo, sambamba na uimarishaji wa programu za kisekta za kuzuia na kupambana na vitendo vya ukatili dhidi ya makundi yote kwa kufanya uchambuzi wa afua zilizoainishwa katika MTAKUWWA wa Pili na kulinganisha na matokeo ya utafiti huu wa pili na hili litasaidia katika kuongeza bajeti na rasilimali watu ili kuzuia ukatili dhidi ya makundi yote na kuboresha huduma kwa manusura wa vitendo vya ukatili.

"Ninaomba kusisitiza kuwa, matokeo haya ya utafiti huu yatawezesha Serikali na Wadau kuboresha na kuandaa Mipango, Programu na Mikakati mbalimbali ya kutokomeza ukatili nchini itakayoimarisha Ulinzi na Usalama wa Watoto na Vijana kwa maslahi mapana ya kizazi cha sasa na cha baadae." amesisitiza Dkt. Gwajima 

Dkt. Gwajima amesema, suala la ukatili dhidi ya watoto na vijana ni la ukiukaji wa haki za binadamu na pia linaleta changamoto kubwa za afya katika jamii na kubadilisha maisha ya watu wanaopitia ukatili. 

Ameongeza kwamba, ukatili huleta athari za muda mrefu za kiafya ikiwa ni pamoja na matatizo ya afya akili, mawazo ya kujiua, tabia hatarishi za ngono, uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa ya zinaa ikiwemo VVU, matumizi ya dawa za kulevya. Pia ukatili hupunguza fursa mbalimbali za kimaendeleo na kuongeza umaskini katika jamii.

Naye Mtakwimu Mkuu wa Serikali kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Amina Msengwa amesema, utafiti huo ni wa Kitaifa ambapo umefanywa katika mikoa 31 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutumia sampuli wakilishi ya Kitaifa hivyo, Takwimu hizo ni bora na zinafaa katika kuweka mipango mikakati na Programu na kufanya tathmini ya kuwalinda Watoto na Vijana dhidi ya Ukatili.



Listen Mkisi Radio