JSON Variables

Saturday, April 26, 2025

BODI YA WAKURUGENZI TASAC YATAKA UFANISI WENYE TIJA YA UWEKEZAJI WA BANDARI

 


NA MWANDISHI WETU, BUKOBA

BODI ya Wakurugenzi  wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limesema kuwa Serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi ya ujenzi wa Bandari za Kemondo na Bukoba hivyo fedha hizo zinatakiwa kuleta tija na zirudi kutokana huduma zitazotolewa na Bandari hizo.


Akizungumza na waandishi wa habari wakati ziara Bodi katika Bandari hizo Mwenyekiti wa Bodi hiyo Nah.Mussa Mandia amesema kuwa baada ya maboresho ya miundombinu ya ujenzi wa bandari watahudumia mizigo na abiria kwa kiwango kikubwa ikilinganishwa na ilivyokuwa awali.


Amessema kuwa fedha ya Bandari ya Kemondo bilioni 20 na ujenzi wake umekamilika ambapo huduma zake zimeongezeka hadi kufikia tani 150000 kwa mwezi na mapato yake yameongezeka mara tatu huku Bandari ya Bukoba ujenzi wake ukiwa katika hatua za mwisho unaogharimu zaidi ya sh.Bilioni 19.


Amesema  kuwa kama wadhibiti ni kuhakikisha Bandari hizo zinaendelea kutoa huduma bora na tija kwa serikali huku akitaka wasimamizi wa bandari kusimamia kwa  weledi.


Amesema Serikali ya awamu ya Sita ya Dkt.Samia Suluhu Hassan imeweza kutimiza ndoto katika upanuzi wa bandari za Kemondo na Bukoba ambayo miundombinu yake ilikuwa ya zamani ambapo haiendani na mahitaji ya sasa.


Hata hivyo amesema kazi bodi itaendelea kushauri katika taasisi wanayoidhibiti ambapo matokeo yake yanaonekana kwa miradi mbalimbali kwenye bandari nchi nzima


Mkuu wa  Bandari ya Bukoba wa TPA Malick Ismail amesema kuwa Bandari hiyo maboresho ya ujenzi bandari hiyo baada ya kukamilika watahudumia meli nne kwa wakati mmoja tofauti na ilivyokuwa awali ambapo walikuwa wakihudumia meli moja. 


WATUMISHI WA UMMA NI TASWIRA YA SERIKALI

 

Watumishi wa umma ni taswira au sura ya Serikali hivyo tunatakiwa tuangalie na kuzingatia namna tunavyofanya kazi na tunapotekeleza majukumu ya Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa niaba ya Serikali. Kila mmoja ana wajibu kwa kutunza taswira ya Serikali tunayoitumikia chini ya Uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Hayo yamesemwa na Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo wakati anafunga mafunzo elekezi kwa watumishi wapya wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali yaliyofanyika Kibaha mkoani Pwani kwa muda wa siku tano.

Bi. Mtulo amewaeleza watumishi hao kuwa Serikali ina sheria, taratibu na kanuni zinawapa mwongozo wa namna ya kufanya kazi kama mtumishi wa umma ambapo katika hayo maadili ya utumishi wa umma, yanatuasa kuhusiana na rushwa. 


“Sisi ni Mawakili wa Serikali, tunaendesha mashauri yenye maslahi mapana ya Serikali ambapo mashauri hayo yana kiwango kikubwa cha fedha na yanahusisha watu mbalimbali ndani na nje ya nchi, hivyo Mawakili wa Serikali tujiepushe na rushwa. Aidha, inapotokea unakutana na mazingira ya rushwa, kimbia ili kulinda taswira ya taasisi na Serikali; heshima, utu na haiba yako kwa jamii na watu wanaokutegemea,” amesisitiza Bi. Mtulo.


Bi. Alice Mtulo amewataka Mawakili hao kutunza siri za Serikali kwa kuwa majukumu wanayotekeleza yanawapa nafasi ya kufahamu taarifa mbali mbali. “Jinsi unavyotunza siri zako, una wajibu wa kutunza siri za Serikali, tuwe waangalifu katika hili.Ukikutwa umevujisha taarifa za Serikali utachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria,” amefafanua Bi. Mtulo.

Aidha, amewaasa Mawakili hao kuzingatia mawasiliano na uhusiano baina yao na viongozi, watumishi wengine na wadau wanaofanya nao kazi. Alisisitiza kuwa na mipaka kwa kuzingatia taratibu za Ofisi ikiwemo kuwa makini kwa yale wanayoandika na kuongea ikiwa ni pamoja na kufuata sheria, kutumia hekima na busara, kuwa waaminifu na wasikivu kwa Serikali tunayoitumikia.

“Sipo tayari kumvumilia mtu yeyote asiyekuwa na nidhamu kwake yeye mwenyewe, wenzake na kwa kiongozi wake.


Vile vile, ametoa rai kwa Mawakili hao kuzingatia na kutumia mifumo ya TEHAMA kwa kuwa Serikali imejikita kwenye matumizi ya mifumo ya TEHAMA. Ofisi ina mifumo mbalimbali ya TEHAMA ambapo kila mtumishi atapimwa utendaji kazi wake kupitia mifumo hiyo. Alisisitiza kila mmoja anapaswa kujaza taarifa za utekelezaji wa majukumu kupitia mifumo hiyo. “Ukitoka Mahakamani jaza taarifa kwenye mifumo husika ili Ofisi ipate takwimu sahihi na kwa wakati.” Aidha alisisitiza kuhusiana na dhumuni na wajibu wa kila mmoja kwa Ofisi, wajibu kwa wafanyakazi wenzako na wajibu kwako wewe binafsi. “Kumbuka na tafakari kuwa ulikuja  Ofisini peke yako, usifuate mikumbo na usiwe mwanaharakati. Zingatia sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa umma, endapo una mahitaji ya msingi wasilisha kwa mamlaka husika kwa utaratibu uliowekwa na  yatafanyiwa kazi,” amefafanua Bi. Mtulo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Ofisi hiyo, Bi. Asha Hayeshi amewaeleza Mawakili hao kuwa ni muhimu kwa Wakili wa Serikali kutekeleza majukumu yake kwa kushirikiana na watumishi wenzake ili kurahisisha mgawanyo wa majukumu na matumizi bora ya ujuzi kwa kila mmoja wakati wa kuandaa majibu ya mashauri ya Serikali, kuchambua ushahidi kwa kina na kuhakikisha mashauri yanaendeshwa kwa ufanisi mkubwa kwa maslahi mapana ya Serikali.

Friday, April 25, 2025

TAIFA LIMEPATA MAFANIKIO MAKUBWA MIAKA 61 YA MUUNGANO-MAJALIWA

 

WAZIRI MKUU,  Kassim Majaliwa amesema Tanzania ni Taifa lililopata mafanikio makubwa katika sekta mbalimbali za maendeleo katika kipindi cha miaka 61 ya Muungano.


Amesema hayo leo (Ijumaa, Aprili 25, 2025) wakati akizungumza na maelfu ya wakazi wa Wilaya ya Ukerewe Mkoani Mwanza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Getrude Mongela. 


Mheshimiwa Majaliwa amefanya ziara ya siku moja katika Wilaya ya Ukerewe ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 61 ya Muungano.

Amesema kuwa Muungano wa Tanzania Bara na Zanzibar umewezesha kujenga Taifa imara na lisiloyumba “Muungano huu umewezesha kuwa na  Taifa ambalo limepata mafanikio katika miradi mbalimbali ya maendeleo Bara na Visiwani, Muungano huu ni tunu ambayo kila mmoja anapaswa kuilinda, kuienzi na kuisemea popote.”


“Kwenu hapa Ukerewe Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mabilioni mengi ya fedha yameletwa kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo katika sekta elimu, afya, maji, mawasiliano na maeneo mengine muhimu. Serikali hii imefanya mabadiliko mengi.”


Kadhalika, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikagua maendeleo ya ujenzi wa mradi wa hospitali ya rufaa ya kibingwa yenye hadhi ya mkoa inayojengwa katika Wilaya ya Ukerewe Mkoani Mwanza.

Akizungumza baada ya kukagua hospitali hiyo Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa hospitali hiyo itawawezesha wakazi wa Wilaya hiyo kutotembea umbali mrefu ikiwemo kwenda  Mwanza kufuata huduma za kibingwa za afya.


Hospitali hiyo inajengwa na Mkandarasi M/S Dimetoclasa Realhope Limited JV Mponela Construction & Co. Ltd kwa gharama ya shilingi bilioni 25.03 na inategemewa kukamilika ifikapo Julai 8, 2026.


Pia, Mheshimiwa Majaliwa ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa jengo la utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza ambalo ujenzi wake utagharimu shilingi bilioni 3.7.


Akizungumzia kuhusu sekta ya maji, Mheshimiwa Majaliwa amewataka Watanzania kuendelea kuwa na imani na Serikali na amewahakikishia kuwa miradi ya maji itatekelezwa kutokana na umuhimu mkubwa wa huduma hiyo kwa jamii.

Akizungumza kuhusu maboresho ya vivuko katika Wilaya ya Ukerewe Meneja Vivuko Kanda ya Ziwa , Vitalis Bilauri amesema Serikali inakamilisha ujenzi wa vivuko vitano ambavyo vitatoa huduma katika Wilaya ya Ukerewe na visiwa vyake.


Naye Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Uhusiano kwa Umma Anselim Namala amesema kuwa Meli ya MV Clarius ipo katika hatua ya ukaguzi ili ukarabati uanze kufanyika.


Pia, ameongeza kuwa ukarabati wa meli ya Mv Butiama umekamilka na sasa upo katika hatua ya mwisho ya ukaguzi na kupata vibali kabla ya kuanza kutoa huduma kwa wananchi hivi karibuni.

Naye, Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dkt. Festo Dugange amesema Ujenzi wa Hospitali Teule ya Rufaa ya Kibingwa yenye hadhi ya Mkoa Wilayani Ukerewe ni hatua kubwa katika utoaji wa huduma za afya katika Wilaya ya Ukelewe na Visiwa Vyake.


"Hospitali hii itakapo kamilika itakuwa ni miongoni mwa hospitali zenye hadhi kubwa za utoaji huduma nchini, Serikali ya Awamu ya sita chini ya Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya makubwa katika sekta ya Afya na Ujenzi wa Hospitali hii ni uthibitisho wa mafanikio hayo."

MAAJABU YA RAIS WA BUKINAFASO KUNUNUA GRADERS 1,000.

 

BREAKING: Rais wa Burkina Faso Kapteni Ibrahim Traoré amenunua Graders zaidi ya 1,000 na magari mbalimbali ili kusaidia juhudi za ujenzi wa barabara kote Nchini Burkina Faso.

Jana, alikabidhi rasmi mitambo hiyo kwa timu zinazohusika na maendeleo na matengenezo ya miundombinu ya barabara nchini humo 

Katika hotuba yake, Captain Traoré alisisitiza umuhimu wa kuwa na barabara bora kutoka mashambani hadi sokoni, akieleza kuwa barabara nzuri zitawawezesha wakulima kusafirisha mazao yao kwenda mijini kwa ufanisi zaidi na bila kuharibika.

Uwekezaji huu mkubwa katika maendeleo ya kitaifa unafanyika licha ya shutuma za awali kutoka kwa Jenerali Langley, ambaye ni Mkuu wa Jeshi la Marekani Kamandi ya Afrika ambaye alidai kuwa Traoré anatumia vibaya akiba ya dhahabu ya nchi ya Burkina Faso kwa manufaa yake binafsi.

MIAKA MINNE YA RAIS SAMIA, ARUMERU YAPOKEA SHILINGI BILIONI 100.6 ZA MAENDELEO

 

 Dkt. Biteko asisitiza Watanzania wasijaribu kuchezea amani

Dkt. Biteko awataka Watanzania kuenzi, kudumisha Muungano 

Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema wananchi wa wilayani Arumeru, mkoani Arusha na Watanzania kwa ujumla wana kila sababu ya kumshukuru na kumuombea Rais Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.


Dkt. Biteko amesema hayo leo Aprili 25, 2025 katika mkutano wa hadhara uliofanyika Tengeru Wilaya ya Arumeru, Mkoa wa Arusha ambapo amesema katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Dkt. Samia wilaya ya Arumeru imepokea zaidi ya shilingi bilioni 100 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

“Arusha DC imepata fedha kiasi cha shilingi bilioni 49.6 na Wilaya ya  Arumeru imepokea zaidi ya shilingi  bilioni 51  kwa ajili ya shughuli na miradi mbalimbali ya maendeleo,” amesema Dkt. Biteko.


Akiwa Wilayani humo amekagua mradi wa kuboresha miundombinu ya Hospitali ya wilaya Arumeru na mradi wa ujenzi wa jengo la utawala la Chuo cha Maendeleo ya Jamii Tengeru ambapo ameeleza kufurahishwa na utekelezaji wa miradi hiyo.

 

Ametoa mfano wa miradi ya maendeleo iliyotekelezwa kuwa ni miradi ya umeme na Tanzania ni kati ya nchi chache barani Afrika ambazo zimefanikiwa kuzalisha umeme kwa asilimia 100.


Miradi mingine iliyotekelezwa ni ujenzi wa shule, maabara, hospitali, vituo vya afya, miradi ya kilimo pamoja na barabara.

Licha ya mafanikio hayo Dkt. Biteko ameeleza kuwa Serikali ni sikivu na itaendelea kutatua changamoto za barabara, maji na madaraja zilizopo mkoani Arusha pamoja na maeneo mengine nchini.


Fauka ya hayo, Dkt. Biteko amewahimiza Watanzania kudumisha amani na mshikamano kwa kuwa ndio msingi wa maendeleo yaliyopatikana.


 “ Tusijaribu kuichezea amani, amani inapaswa kulindwa kwa gharama yoyote. Rais Samia ameapa kuilinda amani hii kwa gharama yeyote. Nitumie nafasi hii kumkumbusha kila Mtanzania kuwa tunu ya amani ndiyo inayofanya tuendelee kuwa salama na bila amani hatuwezi kuwa na chochote,” amesisitiza  Dkt. Biteko.

Ameongeza kuwa katika kuadhimisha miaka 61 ya Muungano, Watanzania waendelee kudumisha amani, umoja na kuwa na mshikamano usioangalia dini, kabila wala itikadi za siasa. Aidha, Muungano ulipo wa Tanganyika na Zanzibar ni  wa kipekee na wenye faida nyingi, huku akitaja kauli mbiu yake kuwa  “Muungano wetu ni Dhamana, Heshima na Tunu ya Taifa; Shiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025”


Vilevile, amewahimiza wananchi kushiriki katika Uchanguzi Mkuu na kumchagua Rais, wabunge na madiwani mwezi Oktoba mwaka huu. 

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Paul Makonda amesema kuwa katika mchoro wa mkoa uliopo kutakuwa na barabara ya  itakayojengwa eneo la Usa River pamoja na arabara kuelekea Uwanja wa Ndege Kisongo ili kupunguza adha ya usafiri kwa wakazi wa Arusha.

Ameendelea kusema kuwa barabara ni ajenda kubwa katika Mkoa huo na kuwapongeza  wananchi kwa kuelewa kuwa maendeleo ni mchakato na kuwa madiwani na wabunge wamekubaliana kipaumbele chao kwa mwaka 2025/26 ni barabara.


Ametoa pongezi kufuatia miradi ya umeme mkoani humo “Tunakushukuru  Naibu Waziri  Mkuu kwa kutuletea mradi wa umeme wa REA na wananchi wanaunganishiwa umeme kwa shilingi 27,000.  Mradi utakaokamilisha umeme katika vijiji na vitongoji vyote kupata umeme katika mkoa wa wetu,” 

Awali akizungumza, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. John Jingu amesema kuwa Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru ni taasisi ya kipekee inayotoa huduma za maendeleo ya jamii nchini ambayo ilianzishwa mwaka 1963.


Ameeendelea kusema kuwa Taasisi hiyo ni tegemeo la kuzalisha wataalamu wa maendeleo ya jamii na inaendelea na ujenzi wa jengo la utawala litakalo gharimu shilingi bilioni 5.6 na hadi sasa wametumia shilingi bilioni 2.7.


“Tuna kila sababu ya kumshukuru Rais Samia kwa kutupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa mradi huu ambao ukikamilika utatatua changamoto ya uhaba wa ofisi kwa kuwa na ofisi 44 zitakazo hudumia watu 94,” amesema Dkt. Jingu.


Aidha, Dkt. Biteko ameendelea na ziara yake siku tano mkoani humo ambapo tayari ametembelea Wilaya za Monduli, Longido na Aumeru ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 61 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

USHIRIKIANO WA ZANZIBAR NA OMAN KUENDELEZA KUIMARIKA KATIKA NYANJA MBALI MBALI

 

Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza ushirikiano na Serikali ya Oman katika nyanja mbali mbali ili kuziletea nchi hizo maendeleo.


Ameyasema hayo Ofisini kwake Mazizini Wilaya ya magharibi B wakati alipokuwa akizungumza na mjumbe kutoka Serikali ya Oman Sheikh Abdullwahab Suleiman alipomtambulisha kuwepo Zanzibar kwa ajili ya kufundisha elimu ya mwezi, nyota na sayari nyengine.


Amesema ni muhimu kwa maulamaa kufahamu elimu hiyo katika kuwasaidia kuzitambua vyema sayari na mwenendo wake ambapo elimu hiyo ina manufaa wakati wa muandamo wa mwezi.


Aidha, Mufti huyo aliwataka Maulamaa hao kuzingatia kwa umakini na kuifahamu elimu hiyo, kwani itawaletea Wazanzibari manufaa kujua masuala ya sayari.


Nae Mtaalam wa maswala ya nyota kutoka Oman Sheikh Abdullwahabi Suleiman amesema ujio wake huo Zanzibar una lengo la kutoa elimu kwa Maulamaa pamoja na Mashekh kutoka Ofisi ya Mufti ili kuweza kufahamu elimu hiyo.


Pia ameishukuru Ofisi ya Mufti mkuu wa Zanzibar kwa mapokezi mazuri ambayo yataleta mshikamano baina ya Serikali hizo kwani Zanzibar na Oman wanaudugu wa muda mrefu.


Mtaalam wa maswala ya nyota na sayari Sheikh Abdulwahabi yupo Zanzibar kwa muda wa wiki moja kwa lengo la kutoa elimu hiyo.

SERIKALI YATOA UPENDELEO KWA MAKUNDI MAALUM KATIKA SHERIA YA UNUNUZI WA UMMA

 


Na Mwandishi wetu

PWANI.


Serikali inatambua umuhimu wa kuwawezesha watu wenye mahitaji Maalum kushiriki katika shughuli za kiuchumi , hivyo kuna upendeleo maalum katika Ununuzi wa Umma kwa ajili yao.


Hayo yamesemwa leo tarehe 25 Aprili, 2025 na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma Bw. Dennis Simba wakati akifungua mafunzo kwa watu wenye mahitaji maalum  katika Ununuzi wa Umma. 

Amesema mafunzo haya yamekusudia kuelimisha na kuhamasisha makundi maalum juu ya haki zao na fursa wanazoweza kuzitumia katika mchakato wa Ununuzi wa Umma hivyo tunataka kuona makundi haya yanapata fursa za kibiashara ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa Nchi. 

"mpaka sasa kuna jumla ya vikundi maalum 280 vilivyokamilisha usajili na uhuishaji wa taarifa zao katika Mfumo wa Ununuzi wa Umma (NeST) ambapo vikundi hivyo vimepata tuzo za mikataba zilizotolewa kwa makundi maalum ambazo jumla ni tuzo Mia Nne Arobaini zenye thamani ya Shilingi Bilioni 15 ambapo Vijana ni vikundi 163 sawa na 58% wanawake ni vikundi 96 sawa na 34% na wenye Mahitaji maalum (Walemavu) ni Vikundi 4 sawa na 2% na wazee Vikundi 17 sawa na 6% sasa kama unavyoona usajili ni mdogo na mahitaji ni kwamba kila kikundi kiwe na kati ya watu watono hadi 20 hivyo bado kunamuamko mdogo kwenye vikundi vya watu wenye mahitaji maalum na ndio maana PPRA tumeona kuna haja ya kukutana na viongozi wa TAB na TLB , Wizara ya Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu pamoja na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ili tuweze kuimarisha jambo hili. Alisema Mkurugenzi Mkuu PPRA 

Aidha  Bw.  Simba amesema, Mamlaka ya Ununuzi wa Umma inajukukumu la kuhakikisha kuwa Mifumo ya Ununuzi inazingatia usawa, haki na uwazi na kutoa mafunzo kwa watu mbalimbali na kuanzisha programu za uhamasishaji na kushirikiana na wadau muhimu ili kuhakikisha kuwa makundi haya maalum yanaelewa haki zao katika michakato ya Ununuzi wa Umma. 

"Nataka kusisitiza kwamba kila mmoja wetu anajukumu la kuhakikisha kuwa anafaidika na fursa zinazotolewa kwa Makundi Maalum katika sekta ya ununuzi wa umma, Mafunzo haya ni mwanzo mzuri wa safari ya kuelewa na kutumia haki hizi katika kuboresha mazingira ya biashara na kuongeza tija katika Uchumi wa nchi, hivyo nitumie fursa hii kuwashukuru kwa kujitolea na kujiunga na mafunzo haya na nimatumaini yangu kuwa mtachukua maarifa haya na kuyatumia katika shughuli zenu za kila siku" Alisistiza Mkurugenzi Dennis Simba

kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wasioona Tanzania Bw. Omary Itambu Amasi amewashukuru PPRA kwa kuwaletea mafunzo ambayo yatawasaidia katika kupata tenda mbalimbali ambazo wengine wasio na mahitaji maalum wanazipata.


" Hapo mwanzo tulishindwa kupata fursa za tenda kutokana na kukosa Elimu hii kwa hiyo leo PPRA mmekuja kutupa mkate au ufunguo ambao utafungua kila kitasa kwenye masuala ya ununuzi katika sekta za Umma hivyo niwapongeze sana lakini sana niwaombe huu sasa ni mzizi mliousimika na mzizi ukianza litakuja shina hatimae matawi maana yangu ni kwamba hiki kilichoanzishwa sasa ni jambo ambalo linahitajika katika maeneo yote 26 Tanzania Bara na niwaombe bajeti zenu zitukumbuke. Alisema Mwenyekiti Huyo. 

Uendeshaji wa mafunzo hayo ni mwendelezo wa Mamlaka wa utoaji mafunzo kuhusu Sheria ya Ununuzi wa Umma na Mfumo wa NeST ili kuwajengea uwezo wadau wote wa sekta hii nyeti nchini.

SERIKALI KUENDELEA KUWEKEZA KATIKA SEKTA YA AFYA - DKT. BITEKO

 

.....................

Dkt. Biteko atambelea Hospitali ya Wilaya ya Meru

Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati

Serikali imeahidi kuendelea kuboresha huduma za Afya nchini katika ngazi zote ili kuboresha huduma za Afya kwa Watanzania.

Hayo yamesemwa Aprili, 25, 2025 na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko akiwa ziarani Mkoani Arusha ambapo amesema kuwa lengo la uwekezaji katika sekta ya afya ni kusigeza huduma za afya kwa wananchi."

Serikali inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea na uwekezaji mkubwa unaofanya kwa kujenga hospitali, vituo vya afya na zahanati katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza baada kutembelea Hospitali ya Wilaya ya Meru, iliyopo Wilaya ya Arumeru, Mkoa wa Arusha, Mhe. Dkt. Biteko amesema lengo la uwekezaji katika sekta ya afya ni kuboresha afya za Watanzania.

“ Kama mnavyofahamu afya ndio mtaji wa wananchi na Serikali itaendelea kuboresha huduma za afya kwa kujenga hospitali mpya na kufanyia ukarabati zilizopo,” amesema Dkt. Biteko.

Amesistiza “ Watu wote nilioongea nao hapa hospitalini wamesema hali ya utoaji huduma imeimarika na ni nzuri, nataka niwaambie Rais Samia katika uongozi wake ameapa kuboresha hali za maisha ya Watanzania. Hapo awali ilimlazimu mgonjwa kutoa makozi siku tatu mfululizo ili kumfanyia kipimo cha ugonjwa wa kifua kikuu, leo tuna mashine ya kisasa inayotumia saa mbili kupata majibu ya mgonjwa,”

Ameendelea kusema ujenzi na maboresho yaliyofanyika hospitalini hapo imetumia raslimali za ndani (force account) na kazi imefanyika kwa ubora na kuzingatia thamani ya fedha.

Ameongeza kuwa katika kuelekea miaka 61 ya Muungano uwepo wa hospitali hiyo ni kiashiria cha kuwa nchi inapiga hatua kimaendeleo. Hivyo, wananchi hawana budi kuuenzi na kuutunza Muungano.

Aidha, amewataka wagonjwa kuwa wavumilivu wanapoenda kupata matibabu huku wakizingatia kuwa wahudumu wa afya wanafanya jitihada kubwa kuwapa huduma bora.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Paul Makonda amesema kuwa wananchi wa eneo hilo wanafurahia huduma nzuri zinazotolewa na sasa idadi ya wagonjwa wanaohudumiwa ni 12,000 kutoka 3,000 ya awali.

Naye, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Meru, Daktari Elisante Fabiani amesema kuwa uboreshaji wa majengo katika hospitali hiyo umesaidia utoaji huduma na kuongeza idadi ya vipimo vya maabara kutoka 18 hadi 32.

“ Tuna mashine ya kisasa ya kupimia vimelea vya kifua kikuu na ndani ya saa mbili pekee mgonjwa anapata majibu ya kifua kikuu na kuanza matibabu na ina uwezo wa kugundua dawa ya kutumia,” ameeleza Daktari Fabian.

Aidha, Dkt. Biteko ameendelea na ziara yake siku tano mkoani humo ambapo ametembelea Wilaya za Longido na Monduli ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 61 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.