JSON Variables

Header Ads Widget

Responsive Advertisement

Jumatatu, 7 Julai 2025

LUHEMEJA AWATAKA WATANZANIA KUTOA UZITO NA MSISITIZO UHIFADHI NA USIMAMIZI WA MAZINGIRA


..............

WATANZANIA wamehimizwa kulipa uzito na msisitizo suala la uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini kwani ni agenda muhimu ya kimaendeleo kwa binadamu.

Hayo yamesemwa leo Jumapili (Julai 6, 2025) Jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Cyprian Luhemeja wakati akizindua Siku ya Mazingira iliyoadhimishwa katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (DITF).

Luhemeja amesema  Dunia inakabiliwa na changamoto za kimazingira zikiwemo ukataji miti, upotevu wa viumbehai, kupanda kwa joto, hivyo jitihada za pamoja baina ya Serikali, Asasi zisizo za Serikali, sekta binafsi na wananchi zinahitajika katika kukabiliana na hali hiyo.

”Natoa rai kwa Watanzania kudumisha utamaduni wa kutunza mazingira kwa kuepuka kutupa taka na kukata miti hovyo. Aidha, tuendeleze utamaduni wa kupanda miti na kupunguza matumizi ya kuni na mkaa kwa kutumia nishati safi ya kupikia” amesema Mhandisi Luhemeja.

Ameongeza kuwa Tanzania imebarikiwa urithi mkubwa wa rasilimali asilia na vivutio vya kipekee vinavyotambulika kitaifa na kimataifa ikiwemo misitu, ukanda wa bahari, uchumi wa bahari, eneo la misitu ya mikoko, hivyo endapo mazingira yataendelea kuharibiwa rasilimali hizo hazitakuwa salama.

Mhandisi Luhemeja awataka wananchi na  wadau kupunguza matumizi ya plastiki kwa kutumia falsafa ya ”Punguza, Tumia Tena na Rejeleza” ambapo kwa mujibu wa tafiti zimebainisha kuwa taka za plastiki huchukua miaka 400 mpaka 1,000 kuoza ardhini na hivyo kuleta athari hasi kwa afya ya binadamu, mazingira na uchumi.

Ameeleza kuwa katika kukabiliana na changamoto za mazingira,  Serikali kwa kushirikiana na wadau imefanya jitihada mbalimbali  ikiwa ni pamoja na kuandaa na kutekeleza Sera ya Taifa ya Mazingira, Mkakati wa Taifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi, Mchango wa Taifa wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Maafa.

Ameeleza kuwa zaidi ya asilimia 90 ya kaya nchini bado zinaendelea kutegemea kuni na mkaa kama chanzo kikuu cha nishati ya kupikia, hivyo Serikali imezindua Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034) unaolenga kuhakikisha kuwa asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.

“Mkakati huu unaonesha dhamira ya kweli ya kumkomboa Mtanzania dhidi ya athari za nishati chafu, hasa wanawake ambao ndio wahanga wakubwa. Hili si suala la majiko au mafuta tu, bali linagusa afya, heshima, fursa na haki ya kuishi katika mazingira bora” amesema Mhandisi Luhemeja.

Awali Mkurugenzi wa Usimamizi wa Biashara wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE), Bi. Lulu Mkudde amesema tukio la uzinduzi wa Siku ya Mazingira ni la kwanza kufanyika tangu shughuli na huduma za maenesho hayo kuanza nchini.

Amesema kuwa TANTRADE itaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais katika masuala ya uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini hususani kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia na upandaji miti.

“Tunatambua suala la uhifadhi wa mazingira kwa sasa limekuwa ni fursa ikiwemo biashara ya kaboni ambayo imeendelea kunufaisha jamii ya Watanzania. Tutaendelea kuunga mkono juhudi hizi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya jamii yetu” amesema Mkudde.

MWISHO

  

0 comments:

Chapisha Maoni

Listen Mkisi Radio