JSON Variables

Thursday, April 24, 2025

DCEA YAKAMATA KG.4,568 YA DAWA ZA KULEVYA,YAZUIA TANI 14 ZA KEMIKALI BASHIRIFU KUINGIA NCHINI

Kamishna Jenerali wa Mamlaka Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) Aretas Lyimo wakati akitoa taarifa kuhusu operesheni ya Mwezi machi hadi April mwaka huu ambayo wameifanya kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola katika mikoa ya Dar es salaam,Shinyanga,Tabora,Songwe,Mbeya na Arusha.
Mkurugenzi Msaidizi Malalamiko kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU ) Thobias Ndaro akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam.

......................

 NA MUSSA KHALID

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imekamata Kilogram 4,568 za dawa mbalimbali za kulevya na kuteketeza ekari 178 za mashamba ya bangi pamoja na kushikilia magari,pikipiki tano na bajaji moja vilivyohusika kwenye uhalifu huo.

Pia imefanikiwa kuzuia tani 14 za kemikali bashirifu zilizokuwa ziingizwe nchini kinyume na sheria pamoja na pakti 10 za pipi zenye uzito wa gramu 174.77

Hayo yameelezwa jijini Dar es salaam na Kamishna Jenerali wa Mamlaka hiyo Aretas Lyimo wakati akitoa taarifa kuhusu operesheni ya Mwezi machi hadi April mwaka huu ambayo wameifanya kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola katika mikoa ya Dar es salaam,Shinyanga,Tabora,Songwe,Mbeya na Arusha.

Kamishna Lyimo amesema kuwa katika operesheni zilizofanyika mkoani Mbeya,raia wa Uganda Herbert Kawalya mwenye hati ya kusafiria Na.B00132399  na mmiliki wa Kampuni ya Hoxx Wells Lux Tour Limo alikamatwa akiwa na pakti 10 za pipi zenye uzito wa gramu 174.77 zilizotengenezwa kwa dawa aina ya bangi yenye kiwango kikubwa cha sumu ya tetrahydrocannabinol (THC).

“Aidha katika tukio lingine Mkoani Mbeya zilikamatwa kilogram 1658 za bangi aina ya skanka na kilogram 128.7 za bangi zilizokuwa zinaingizwa nchini kutoka Malawi’amesema Kamishna Lyimo

Ameendelea kusema kuwa katika operesheni waliyoifanya jijini Dar es salaam,zilifanikisha ukamataji wa kilogram 220.67 za bangi aina ya skanka katika kata yaChanika zikiwa zimefichwa chooni huku kilogram 11 zikikamatwa eneo la ukaguzi wa mizigo kwenye bandari ya kuelekea Zanzibar

“Katika operesheni zilizofanyika mikoa ya Arusha,Tanga na Manyara zilikamatwa Kilogram 733.74 za dawa za kulenya aina ya Methamphetamine,kilogram 91.61 za heroin,kilogram 692.84 za mirungi iliyokuwa inaingizwa kutokea nchini Kenya na Kilogram 115.05 za bangi pamoja na kuteketeza ekari mbili za mashamba ya bangi’amesema Kamishna Lyimo

Vilevile Kamisha Lyimo amesema katika operesheni zilizofanyika Wilaya ya Uyui na Nzega mkoani Tabora,Kilogram 845 za bangi zilikamatwa na ekari za mashamba ya bangi ziliteketezwa.

Katika hatua nyingie Kamishna Jenerali Lyimo ametoa wito kwa watendaji wa serikali za mitaa kudhibiti uhalifu huo katika maeneo yao na watachukuliwa hatua endapo watashindwa kukomesha na wakibainika kuhusika katika uhalifu huo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Malalamiko kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU ) Thobias Ndaro amesema watahakikisha wanafuatilia kwa umakini watumishi wa umma ambao wanachangia au kuenea kwa changamoto ya dawa za kulenya nchini.

Ametumia fursa hiyo kutoa wito wa watumishi wa umma kuwa waadilifu kwa kutochangia madawa ya kulevya kushamiri katika maeneo yao.

Hata hivyo wazazi na walezi mnahimizwa kuwa makini na kufuatilia kwa karibu mienendo ya watoto wenu ikiwa ni pamoja na kuwaasa wajiepushe na mazingira na sababu zozote zinazoweza kuwaingiza kwenye matumizi ya dawa za kulevya.


WAZIRI MKUU: SERIKALI KUENDELEZA MABONDE NCHINI

 

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea na mpango wa kuyaendeleza mabonde nchini kwa kuyatumia kutoa huduma za kijamii ikiwemo upatikanaji wa maji na nishati ikiwa ni mkakati wa kukabiliana na mafuriko.

 

Amesema moja ya mkakati uliochukuliwa na Serikali ni kuunda mamlaka za mabonde zenye wajibu wa kufanya ufuatiliaji wa mwenendo upitishaji maji na kuratibu namna nzuri ya utumiaji wa mabonde hayo.

 

Amesema hayo leo (Alhamisi, Aprili 24, 2025) wakati akijibu swali la mbunge wa Kyela, Ally Anyigugile Jumbe aliyetaka kufahamu mpango wa Serikali wa kukabiliana na mafuriko nchini, wakati wa kipindi cha Maswali ya Wabunge kwa Waziri Mkuu.

 

“Kama ambavyo tumeona kwenye bonde la mto Rufiji, tumeamua kuanzisha mradi mkubwa sana wa kuzalisha umeme. Nilifanya ziara mkoani Morogoro ambapo tunachimba bwawa kubwa ambalo linategemea maji ya mto Ruvu; ujenzi wa mabwawa haya yataleta maslahi kwa Watanzania ikiwemo kwenye sekta za kilimo, nishati, maji na mifugo.”

 

Ameongeza kuwa mpango wa Serikali ni kuhakikisha inaongeza bajeti kwenye Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maji pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira). “Tunataka kuhakikisha maji yanayosababishwa na mvua hayapotei bure bali tunayatumia kwa faida ya Watanzania.”

 

Aidha, Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kusimamia maslahi ya watumishi, mishahara na madai mbalimbali ili kuhakikisha yanalipwa kwa wakati na waweze kuendesha maisha yao.

 

Amesema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Moshi Mjini, Priscus Jacob Tarimo aliyetaka kufahamu mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wafanyakazi wa kada na elimu zinazofanana wanapata mshahara unaofanana.

 

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali imeanzisha idara ambayo inashughulikia mishahara, posho na marupurupu inayofanya mapitio kila mwaka na kuona mabadiliko ya kiuchumi ya nchi kama yanakwenda sambamba na pato ambalo linamuwezesha mtumishi wa umma kutekeleza majukumu yake.

 

Akitoa ufafanuzi kuhusu mikakati ya Serikali wa kukabiliana na ukatili kwenye jamii, Waziri Mkuu amesema Serikali inatekeleza mipango mbalimbali ya kudhibiti masuala ya ukatili ikiwemo kutoa elimu pamoja na kushirikiana na wadau na taasisi zinazopinga ukatili.

 

Ametoa ufafanuzi huo wakati akijibu swali la Stella Simon Fiyao (Viti Maalum) aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuandaa vitengo maalum shuleni, vyuoni, ngazi za jamii na kwenye ofisi ili kusaidia kukabiliana na vitendo vya ukatili.

 

Mheshimiwa Majaliwa aliongeza kuwa katika kuhakikikisha nchi inakuwa salama dhidi ya ukatili kwenye jamii, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliunda wizara maalum inayosimamia masuala ya kijamii pamoja na kuhakikisha inakabiliana na ukatili kwenye jamii. 

 

“Wizara hii kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeweka mifumo ya kisheria inayomlinda kila mmoja dhidi ya ukatili wa aina yoyote ile. Tumeandaa madawati ya jinsia kwenye taasisi zote za umma ikiwemo shuleni, vyuoni pamoja na kwenye taasisi zinazotoa huduma za kiulinzi kama Jeshi la Polisi na Magereza.”

 

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amesema pamoja na jitihada hizo, kila Mtanzania anapaswa kuwa mlinzi dhidi ya ukatili kwenye jamii. “Matukio haya ambayo yanajitokeza katika jamii, yanaondoa haki ya msingi ya kibinadamu pale anapotendewa ukatili dhidi yake na hivyo kila mmoja awe mlinzi wa matendo haya popote pale.”

TEF YAWAPA POLE WAKATOLIKI KIFO CHA PAPA


...................

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limepokea kwa huzuni na masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis, alifariki dunia siku ya Jumatatu, tarehe 21 Aprili 2025, akiwa na umri wa miaka 88.

Kwa mujibu wa taarifa ambayo imetolewa na Mwenyekiti wa Jukwaa hilo Deodatus Balile imesema Katika kipindi cha miaka 12 ya uongozi wake kama Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kujenga maelewano ya kidini duniani, hususan kupitia juhudi zake za kuhimiza mazungumzo ya amani miongoni mwa dini mbalimbali.


 

Mbeto atoa wito akiwataka wananchi wakatae kuzugwa na Siasa za Kijinamizi

 


 Na Mwandishi  Wetu, Zanzibar 

Chama Cha Mapinduzi (CCM)  kimewataka watanzania kutokubali kuzugwa  kwa namna yoyote na majaribu ya Siasa za  kijinimizi zisizoitakia mema nchi yetu zenye zana  ya  kupoteza ustawi wa Amani na Umoja wa Kitaifa 


Chama hicho  pia  kimesisitiza na kutaja Amani, Utulivu na Mshikamano uliopo Tanzzania  kwa miaka sitini,  umekuwa ukiwashangaza walimwengu  wengi  duniani.


Hayo yametamkwa na Katibu  wa Kamati  Maalum  ya NEC  Zanziabr , Idara ya Itikadi , Uenezi na Mafunzo ,Khamis  Mbeto  Khamis  , aliyewahimiza Watanzania kuendelea kudumisha Amani , Umoja  na Mshikamano wa Kitaifa .


Mbeto  alisema kumekuwa na juhudi  za chini kwa chini kwa muda mrefu,  zinazofanywa na baadhi ya maadui wa Umoja Amani ,  ambao wamekuwa wakijaribu  kutaka  kuvuruga Umoja miongoni  mwa Watanzania 


Alisema kuna baadhi ya Wanasiasa na  Wanaharakati   wakiwemo baadhi ya  watu wazima hovyo   , wamekuwa wakitamani kuliparaganya  Taifa kwa kutanguliza maslahi  yao  binafsi  na kutojali  kabisa  maslahi  ya Umma.


Aliongeza kusema watu hao  wamekuwa wakifanya majaribu kadhaa ikiwemo  kukosoa   Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ,wakitumia  Ukabila, Ukanda na Udini lakini kutokana na msimamo  imara wa Watanzania , mitazamo   yote hiyo  batili imejikuta ikigonga mwamba.


"Chama  chetu kwa heshima  zote   kinawaasa na kuwataka wananchi  kutofuata mkumbo utakaopoteza Amani na Utulivu . Tunajua kuna  vitimbakwiri wachache wanaotumia mgongo wa  Demokrasia iliopo ili  kutimiza  ndoto zao haramu  " Alisema  Mbeto. 


Katibu huyo Mwenezi  aliongeza kusema   ni vema Watanzania wakakataa  kuzugwa na Wanasiasa  ambao  wamekuwa wakitoa matamshi yenye  kuitia shaka na hofu katika  jamii.


"Mataifa mengi  hususan  Barani Afrika  yameshavurugwa na kujikuta yakikumbwa na mapigano ya kijamii   yasiokwisha . Nchi kadhaa zimekuwa zikimwaga damu   wenyewe kwa wenyewe .Mataifa mengine hadi  hayajarudisha maelewano  thabit   "Alieleza


Mbeto  alisema  kutokana na utamaduni  wa watanzania kuwa waamifu kwa nchi yao  ,tunaamini  hakuna  jambo lolote  gumu  lisilozungumzika  ,hivyo    hapajawa na   haja kwa baadhi ya watu kutumia lugha za kibabe na  vitisho.


"Rais Mstaafu Jakaya Kikwete  amewahi kutukanya tusigombanie fito wakati  wote  tunajenga nyumba  moja . Maneno  haya ya dhahabu hayapaswi kupuuzwa kwani ni nadra  kuyasikia    " Alisiaitiza Mbeto 


Aidha, alisema watanzania wana wajibu wa  kuwabaini mapema Wanasiasa wa aina hiyo ambao  wamekuwa wakihaha  usiku na mchana kutaka kulizamisha Taifa letu  kwenye  bwawa la matope ya machafuko na mgawanyiko .


"Lazima tuwafichue   na kukwepa hila , ukorofi na matamshi yao  yenye ishara  mbaya  katika jamii yetu  . Maneno siku zote    hunena kuliko  vitendo. Tusimame imara  kupinga tishio lolote  la kutugawa kwa namna yoyote   " Alisema Mbeto

WASIRA: VIONGOZI WA DINI WAMETUTIA NGUVU KUENDELEA NA UCHAGUZI MKUU*

 

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimewashukuru na kuwapongeza viongozi wa dini kwa ushauri kuhakikisha Nchi inaendelea kuwa na amani hususan kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu na kubariki uchaguzi huo uendelee huku, ikisisitiza kuwa haidharau maoni yanayotolewa.


CCM imesisitiza kuwa haipuuzi ushauri mbalimbali unaotolewa kuelekea uchaguzi huo, lakini imesisitiza hautaahirishwa kwa kuwa mageuzi na mabadiliko ni jambo endelevu na haiwezi kuwa hoja ya kuahirisha uchaguzi.

Hayo yalielezwa leo Chamwino mkoani Dodoma na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara,  Stephen Wasira alipokuwa akipokea taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020-2025 akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake mkoani humo.


"Uchaguzi utaendelea sio kwamba tunapuuza mawazo, tutaendelea kuzungumza mambo ambayo yanaendelea, na tunashukuru sana nchi imetulia. Viongozi wetu wa kiroho wametuongoza wametupa ushauri mzuri sana na mimi nashukuru sana kwa kututia moyo na kutuambia uchaguzi uendelee lakini kwa amani," alisema.

Wasira alisema CCM ni Chama kinachozungumza na kuhimiza amani ndio maana taifa limekuwa na utulivu kwa miaka 60, alisisitiza kwamba hilo linafanya Chama kijivunie kwa kuwa ni ushahidi kwamba kinaweza kusimamia amani.


Alisisitiza haki iko ndani ya amani na kwamba ukiondoa amani utavunja haki za watu wengi hususan wanyonge, "ukiondoa amani watakaoumia hasa ni wanawake, watoto na walemavu."


"Amani ni lazima sasa kuna wanaosema haki, na sisi tunasema ndani ya amani kuna haki, na haki hiyo inalindwa na amani kwa sababu ukiiondoa watu wengi wataathirika wala sio mtu mmoja ni wengi sana na ushahidi wake upo, sisi tumepokea wakimbizi maelfu kutokana na kuvunjia kwa amani kwa majirani zetu," alisisitiza.



HAYA HAPA MAGAZETI YA LEO TAREHE 24.04.2025

 Good morning, Habari gani popote ulipo mdau wetu na msomaji wetu wa mkisi digital, Nikukaribishe kwa bashasha kubwa sana kupitia vichwa vya habari vilivyo pata nafasi katika kurasa za mbele ya magazeti ya leo tarehe 24.04.2025









Wednesday, April 23, 2025

DKT. NCHEMBA ATETA NA MKURUGENZI MTENDAJI WA UENDESHAJI WA BENKI YA DUNIA, JIJINI WASHINGTON

 

Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba Mb), amekutana na kufanya Mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji wa Masuala ya Utawala na Uendeshaji wa Benki ya Dunia, Bi. Anna Bjerde, kando ya Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya IMF na Benki ya Dunia, inayofanyika Jijini Washington D.C, nchini Marekani, ambapo pamoja na mambo mengine, Dkt. Nchemba aliishukuru Benki hiyo kwa mchango mkubwa wa maendeleo ya Tanzania kupitia miradi mbalimbali inayopata fedha kutoka Taasisi hiyo pamoja na kuonesha nia ya kusaidia ujenzi wa Mradi wa Reli ya kisasa (SGR)


Aidha, katika kikao hicho, alitambulishwa Makamu wa Rais Mpya wa Benki ya Dunia anayesimamia Kanda ya Afrika Mashariki na Kusini, Bw. Ndiamé Diop, ambaye ameteuliwa hivi karibuni baada ya Bi. Victoria Kwakwa kumaliza muda wake.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Mhe. Dkt. Elsie Kanza, Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa, Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, Kamishna Msaidizi kutoka Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Fedha, Bw. Robert Mtengule, Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Bw. Nathan Belete na viongozi wengine waandamizi wa Serikali na Benki ya Dunia.


NJE SPORTS YATINGA ROBO FAINALI KWA KISHINDO, YAILAZA TPDC 36-23

 

Timu ya netiboli ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (NJE Sports) imeendelea kung’ara katika michezo ya Mei Mosi kwa kuibuka na ushindi wa mabao 36-23 dhidi ya TPDC, katika mchezo uliopigwa kwenye viwanja vya Mwenge, mkoani Singida.


Mchezo huo ulianza kwa kasi, huku NJE Sports wakionyesha ubora wa hali ya juu na kumaliza kipindi cha kwanza wakiongoza kwa mabao 19-13. Kipindi cha pili walizidi kuimarika, wakiboresha safu ya ulinzi na kushambulia kwa ufanisi zaidi.


Akizungumza baada ya mchezo, Kocha wa NJE Sports, Bw. Mathew Kambona, amewapongeza wachezaji wake kwa kujituma na kufuata maelekezo. “Tunajipanga upya kwa hatua inayofuata, tukilenga kuongeza kasi na nidhamu ya ushindi,” alisema.


Kwa matokeo hayo, NJE Sports imefuzu rasmi hatua ya robo fainali katika mashindano hayo ya kitaifa yanayoshirikisha timu kutoka wizara na taasisi mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani.