Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila amezindua mpango wa ufanyaji biashara kwa saa 24 kwenye soko la Mbezi eneo la stendi ya Malamba Mawili wilayani Ubungo na kuwahakikishia usalama wafanyabiashara huku akiwataka maafisa biashara kutowaonea wafanyabiashara
Akizungza wilayani Ubungo Jijini Dar es salaam katika uzinduzi huo uliofanyika usiku wa kuamkia leo kwenye soko la mbezi mbele ya mamia ya wafanyabiashara wa Soko hilo waliokusanyika kumsikiliza Mkuu wa Mkoa huyo amesema jiji hilo ni kitovu cha biashara inayochagizwa na uwepo wa bandari,kituo cha mabasi cha Magufuli na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwl Nyerere hivyo hakuna sababu ya kulala
Aidha RC Chalamila amewataka wafanyabiashara kutohofia usalama wao kwani Serikali Mkoani humo inazidi kuimarisha ulinzi na usalama ili jiji hilo liwe na amani zaidi huku akimuagiza mkuu wa wilaya ya Ubungo kutoruhusu maafisa biashara kuwaonea wafanyabiashara hao kwani vitendo hivyo ni kinyume na utaratibu
Hata hivyo RC Chalamila ametumia nafasi hiyo kuitaka Halmashauri ya Ubungo kutengeneza vizimba vya mfano vya kufanyia biashara ambapo ametoa muda wa wiki moja kukamilisha kazi hiyo ili wafanyabiashara wenyewe watengeneze vizimba vyao
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Wakili Albert Msando amewahakikishia usalama wafanya biashara, madereva pamoja na wananchi huku Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Hassan Mkwawa akiwahakikishia kuwa pamoja na taa zilizofungwa kwenye maeneo mengi wataendelea kuweka taa za kutosha ili biashara ifanyike saa 24 kwa ufanisi
Shamra shamra za uzinduzi huo zimefanyika usiku mzima hadi asubuhi huku jukwaa likipendezeshwa na wasanii mbalimbali pamoja na Rdj kutoka Efm redio amkiambatana na MC Pilau kutoka Efm.
0 comments:
Post a Comment