JSON Variables

Header Ads Widget

Responsive Advertisement

Jumatatu, 16 Juni 2025

TRA WAAGIZWA KUFUATA SHERIA NA TARATIBU ZA UTUMISHI WA UMMA

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb) akijibu swali bungeni jijini Dodoma.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano, WF - Dodoma)

................

Na Farida Ramadhani, WF – Dodoma

Serikali imemwagiza Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuhakikisha kuwa watumishi wa Mamlaka hiyo wanafuata taratibu na sheria zilizowekwa.

Agizo hilo limetolewa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb)alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Mhe. Janejelly Ntate aliyeeleza kuwa Sheria ya Usimamizi wa Kodi haitekelezwi kwa wafanyabiashara ambao wamesajiliwa kwa mara kwanza na wanatakiwa kulipa jumla ya kodi aliyoahirishiwa baada ya miezi sita (6) kwa awamu tatu.

Mhe. Ntate alisema wafanyabiashara bado wanalipwa kabla ya miezi sita kinyume na matakwa ya sheria hiyo.

Mhe. Chande Serikali kupitia Bunge, ilifanya marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Kodi (Tax Administration Act, 2015) Kifungu cha 22, ili kuahirisha wajibu wa kulipa kodi ya awamu chini ya Sheria ya Kodi ya Mapato kwa kipindi cha miezi sita (6) tangu tarehe ambayo Nambari ya Utambulisho wa Mlipaji (TIN) ilipotolewa kwa mtu yeyote anayesajiliwa na kupewa TIN kwa mara ya kwanza.

“Lengo la mabadiliko hayo ya Sheria ni kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara na wawekezaji”, alibainisha.
Mhe. Chande alisisitiza kuwa kwa wale ambao hawatofuata sheria na taratibu , Sheria ya kiutumishi itachukua mkondo wake.

Wakati huo huo, Mhe. Chande iliwatoa hofu wananchi kuwa “Single Window” haitasababisha uzoroteshaji wa ukusanyaji mapato ya Serikali bali utasaidia kuondoa usumbufu kwa wateja na kurahisisha ukokotoaji wa kodi mbalimbali kupitia Mfumo wa TANCIS uliohuishwa.

Alisema hayo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kondo, Mhe. Mohamed Said Issa aliyetaka kujua changamoto zinazoweza kuzorotesha ukusanyaji wa mapato katika mfumo mpya wa kuchakata kodi ya forodha ambao ni "single window"

Mhe. Chande alisema “Single Window” ni dirisha moja la kufanikisha uwasilishaji wa nyaraka mbalimbali kutoka kwa wadau wote muhimu katika mnyororo wa ugomboaji mizigo Forodha.

Alibainisha kuwa kabla ya mfumo huo, mteja alilazimika kuwasilisha nyaraka na vielelezo mbalimbali kwenda kila idara ya Serikali inayohusika katika mnyororo wa ugomboaji wa mizigo na hivyo kusababisha usumbufu mkubwa na kuchelewesha ugomboaji wa mizigo forodhani.

0 comments:

Chapisha Maoni

Listen Mkisi Radio