Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameiagiza Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kutafuta wawekezaji wazuri watakaoviendesha viwanja vya michezo kwa ubora na ufanisi.
Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo alipovizindua rasmi Viwanja vya Michezo vya Maisara Sports Complex vilivyopo Maisara, Mkoa wa Mjini Magharibi tarehe 16 Mei 2025.
Aidha, amesema kuwa Zanzibar sasa haina sababu tena ya kushindwa kuendesha michezo yoyote kutokana na ukosefu wa viwanja, kwani tayari viwanja vya kisasa na vya kutosha vimejengwa vyenye michezo mchanganyiko 10, ikiwemo: viwanja viwili vya tenisi, viwili vya mchezo wa padel, viwili vya mpira wa miguu, na vinne vya michezo mchanganyiko kama mpira wa kikapu, mpira wa mikono, pete na wavu.
Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi ameagiza viwanja hivyo vitunzwe ipasavyo ili vibaki katika ubora wake wakati wote na viweze kutumika kwa muda mrefu.
Viwanja vya Maisara Sports Complex vimejengwa na fedha za Serikali kupitia kampuni ya Reform Sports kutoka Uturuki kwa gharama ya Shilingi Bilioni 7.
Uzinduzi huo uliambatana na mechi ya kirafiki iliyochezwa viwanjani hapo kati ya Ramsquad na Miembeni, ambapo Miembeni iliibuka mshindi kwa magoli ya penati 5-3.
0 comments:
Chapisha Maoni