Na Mwandishi Wetu
MHADHIRI wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Shule ya Madini na
Jiosayansi , Profesa Evelyne Mbede amesema matumizi ya Nishati Jadidifu
yamesaidia kupunguza vifo vya watoto wanaozaliwa kabla ya miezi yao kutimia
(njiti).
Profesa Mbede ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye Maadhimisho
ya Wiki ya Kitaifa ya Nishati Jadidifu aliyasema hayo Mei 29, 2025 wakati
akifunga maadhimisho hayo yaliyofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa
cha Julius Nyerere (JNICC) jijini
Dar es Salaam.
“Zamani wajawazito walikuwa wakijifungua kwa shida vijijini kutokana
na kukosa umeme hadi kusababisha watoto waliozaliwa chini ya muda wao (njiti)
kupoteza maisha lakini leo hii kwa kutumia nishati jadidifu imesaidia kuokoa
maisha ya watoto hao,” alisema Mbede.
Alisema nishati jadidifu hivi sasa inatumika katika vituo vya afya
na zahanati mbalimbali nchini na si kwa Tanzania tu bali dunia nzima kusaidia
nishati ya umeme kwenye vituo hivyo muhimu kwa jamii.
Profesa Mdebe alisema kumalizika kwa maadhimisho hayo ndio mwanzo
wa maandalizi ya maadhimisho ya msimu mwingine wa 2026 mwakani.
Alisema maadhimisho hayo yamekuwa yakipanua wigo wa ubunifu, kwani
vijana wengi wamekuwa wakiibuka na bunifu mbalimbali na kuongeza matumizi ya
nishati jadidifu na kusaidia maeneo yenye uhitaji, ambako hakuna umeme wa
TANESCO na REA na kutatua changamoto za wananchi.
Profesa huyo alisema Tanzania kushiriki katika maadhimisho hayo ni
kuendana na hali ya mazingira dunia ili kufikia malengo ya 2030 ya kukabiliana
na tabianchi.
“Maonesho haya yanatija sana, kama nchi tumetoka mbali
zamani tulikuwa tukitegemea umeme wa Tanesco pekee lakini hivi sasa tunazalisha
umeme kwa kutumia vifaa mbalimbali na hii ni hatua kubwa,” alisema Mbede.
Maadhimisho hayo yaliandaliwa na Jumuiya ya Wadau wa Nishati Jadidifu Tanzania (TAREA) kwa
kushirikiana na Wizara ya Madini na wadau mbalimbali wa sekta hiyo.
0 comments:
Chapisha Maoni