JSON Variables

Friday, May 9, 2025

RAIS MWINYI:ZANZIBAR ITAENDELEA KUIMARISHA USHIRIKIANO NA MSUMBIJI


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt, Hussein Ali Mwinyi amesema  Zanzibar itaendelea   kuimarisha Ushirikiano  wa kiuchumi na Diplomasia na Msumbiji kwa manufaa ya Nchi hizo mbili.


Rais Dkt.Mwinyi amesema hayo alipokuwa na Mazungumzo na Rais wa Msumbiji Daniel Francisco Chapo  ambaye yupo nchini kwa ziara maalum yaliofanyika Ikulu, Zanzibar tarehe 9 Mei 2025.


Aidha Rais Dkt.Mwinyi ameeleza kuwa uamuzi wa kufanya ziara ya Kwanza Tanzania ikiwemo Zanzibar  baada ya kuchaguliwa kunaonesha kuthamini Ushirikiano huo ulioasisiwa na Viongozi  Waasisi wa Mataifa hayo.


Halikadhalika Rais Dkt, Mwinyi amebainisha Maeneo Matano ya kiuchumi ambayo nchi hizo zinaweza kushirikiana kuwa ni Uchumi wa Buluu, Mafuta na Gesi, Uvuvi wa Bahari Kuu, Utalii na Uwekezaji .


Ameeleza kuwa Uzoefu wa Msumbiji katika  sekta ya Mafuta na Gesi ni eneo muhimu la Kiuchumi ambalo Zanzibar inaweza kujifunza kupitia Uzoefu huo wa takribani miaka 20 wa Msumbiji katika sekta hiyo .


Vilevile Rais Dkt,Mwinyi ameeleza kuwa Mafanikio ya  Zanzibar katika Sekta ya Uchumi wa Buluu nayo ni Sekta Muhimu ambayo Msumbiji inaweza   kujifunza kutokana na Mafanikio ya sekta hiyo hapa nchini.

Akizungumzia Lugha ya Kiswahili  Dkt, Mwinyi amesema ni fursa nyengine muhimu ya Ushirikiano  itakayowezesha nchi hizo kubadilishana Walimu kwa Zanzibar kutoa Walimu wa Kiswahili na Msumbiji kutoa Walimu wa Lugha ya Kireno kujifunza hatua ikayochangia kuchochea Utalii kwa nchi hizo .


Kwa upande mwingine Rais Dkt,Mwinyi ameihakikishia Msumbiji kuwa  Serikali itaendelea kutoa Ushirikiano wa kutosha kwa Wananchi wenye asili ya Msumbiji Waliopo Zanzibar wanaofikia 3000 ambao tayari wengine wameshapewa Uraia wa Tanzania.

Naye Rais Daniel Fransisco Chapo amesema Msumbiji ina dhamira ya dhati ya Kuimarisha Ushirikiano na Zanzibar na ziara yake imelenga kukamilisha azma. hiyo.


Rais Chapo ameeleza kuwa ziara hiyo itafungua milango na fursa za Kiuchumi baina ya nchi hizo pamoja Uhusiamo wa kidiplomasia wa muda mrefu.


Ameipongeza Zanzibar kwa mafanikio inayoyapata kupitia Sekta ya Utalii na Uchumi wa Buluu na kwamba Msumbiji ina kila sababu ya Kujifunza.


Alizungumzia Sekta ya Mafuta na Gesi amesema  Msumbiji imepiga hatua kubwa katika Maendeleo ya Sekta hiyo na  kuihakikishia Zanzibar  kuwa Nchi yake ipo tayari  kubadilishana uzoefu katika sekta hiyo kwa Kuwa na mazungumzo na timu za Watendaji wa pande zote mbili.

AWAMU YA TATU YA MRADI WA MAABARA WA (EAC) WAZINDULIWA LEO, NAIBU WAZIRI WA AFYADKT. GODWIN MOLLEL AKISHIRIKI KATIKA UZINDUZI HUO.


 Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel ameshiriki katika uzinduzi wa Awamu ya Tatu ya Mradi wa Mtandao wa Maabara wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC Mobile Labaratory Project Phase III) uliofanyika tarehe 9 Mei, 2025 katika Makao Makuu ya EAC jijini Arusha kando ya Mkutano wa 25 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wa Afya wa Jumuiya hiyo.


Mradi huo unaolenga kuimarisha uwezo wa nchi wanachama kukabiliana na milipuko ya magonjwa na dharura za afya kwa njia ya uchunguzi wa haraka wa maabara sambamba na kuwajengea uwezo wataalam wa maabara katika nchi wanachama za EAC.

Viongozi wengine waliombatana na Dkt. Mollel katika uzinduzi huo ni: Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia anayeshughulikia masuala ya sayansi, Prof. Daniel Mushi, Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Grace Magembe na maafisa waandamizi kutoka katika Wizara, Idara na taasisi za Serikali Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ya Mapinduzi Zanzibar.


Aidha, katika awamu ya kwanza na ya pili ya mradi huo Tanzania ilinufaika kwa kupata vifaa na mafunzo ya kitaalam, maabara mbili za afya zinazotembea (Mobile Laboratories) na kuimarisha mifumo ya taarifa na uhifadhi wa sampuli.

Tanzania inaendelea kushirikiana na nchi wanachama kuimarisha mifumo ya afya ya kikanda ili kuyafikia malengo yaliyowekwa ya kuwazesha wananchi kupata huduma bora za afya na zenye uhakika.

MUENDELEZO WA ZIARA YA KAMATI YA SIASA CCM MKOA DAR ES SALAAM KUKAGUA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM KWA MIRADI YA KIJAMII NA MIRADI YA MAENDELEO

 

📍Ubungo

🗓08 May 2025


Abasi Mtemvu Mwenyekiti wa CCM Mkoa ameongozana na wajumbe wa kamati ya siasa ya mkoa katika Ukaguzi utekelezaji wa ilani ya CCM Wilaya ya Ubungo.  Mwenyekiti *Mtemvu* amewapongeza watendaji wa serikali katika kutekeleza miradi hiyo na amewasisitiza wananchi kutunza miradi hiyo ambayo imetumia gharama kubwa kwa ajili ya maendeleo ya wana Ubungo. Miradi iliyokaguliwa ni:- 


🎤 ~*Mradi wa maji wa booster* (DAWASA)- KIBAMBA ambao unagharimu *Tsh Bilioni 36.9* ambapo mradi huo unatarajia kunufaisha zaidi ya wananchi takribani *77000* wa wilaya ya ubungo, Temeke na Ilala kwani maji yatakuwa yanatoka mara mbili kwa wiki

🎤~*Mradi wa ujenzi wa vyumba 4 vya madarasa na matundu 8 ya vyoo* katika shule ya sekondari ya Mbezi Inn, ambapo mradi huo umegharimu *Tsh milioni 114* mpaka kukamilika kwake

 


🎤~*Mradi wa ujenzi wa uboreshaji wa kituo cha afya makulumla* ambao unatekelezwa kwa pesa za ndani kwa gharama ya *Tsh milioni 380* ambao ulianza 2022 na unatarajiwa kukamilika mapema tarehe 1/6/2025 ambapo mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar Es salaam ndugu *Abasi Mtemvu* amewasihi mafundi katika mradi huu kufanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha haraka mradi huu.

🎤~ *Mradi wa ufungaji wa Ufungaji wa Transforma 4* kubwa kituo cha umeme cha NIT ambao unafadhiliwa na pesa za ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa gharama ya *Tsh Bilioni 125* ambapo unatarajiwa kukamilika tarehe 3/11/2025 kwani vifaa vimekamilika kwa 95%


Kadhalika; Mkuu wa mkoa wa Dar Es salaam ndugu *Albert Chalamila* ameijulisha kamati ya siasa ya CCM mkoa wa Dar Es salaam kuwa ameziagiza Halmashauri zote zinazounda mkoa wa Dar Es salaam kuhakikisha *zinatenga Fedha ili kujenga vituo vya polisi kwa kushirikiana na jeshi la polisi* ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuendelea kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao ndani ya jiji la Dar Es salaam.

Pongezi kwa serikali ya awamu ya sita chini ya Uongozi  wa Rais *Dkt Samia Suluhu Hassan* kwa kuendelea kusogeza huduma za kijamii kwa wananchi wa Ubungo


*Imetolewa na Idara ya siasa na uenezi mkoa wa Dar Es saalam*


#Ccm Imara

#Kaziiendelee

# DktSamiaMitanoTena🖐🏿


©️Kazi na Utu Tunasonga mbele 2025

WAZIRI MAVUNDE AZINDUA TAARIFA YA UCHAMBUZI UONGEZAJI THAMANI MADINI MUHIMU TANZANIA


◾️ Asema Tanzania imeanza Safari ya Mageuzi ya Sekta ya Madini kuchochea ukuaji wa viwanda. 


◾️ Asisitiza dhamira ya Tanzania kuwa kitovu cha bidhaa zitokanazo na madini muhimu. 


◾️ Balozi wa Uingereza nchini asema hatua hiyo ni kielelezo cha ushirikiano kati ya Tanzania na Uingereza. 


📍 *Dodoma*


Waziri wa Madini Mhe.  Anthony Mavunde ameeleza kuwa, Serikali ya Tanzania imeendelea kuchukua hatua madhubuti kuelekea mageuzi ya kweli ya Sekta ya Madini hapa nchini kwa kuanza rasmi mkakati wa kuongeza thamani ya madini muhimu yanayopatikana nchini. 


Alieleza hayo Mei 8, 2025  wakati akizindua rasmi  Taarifa ya Uchambuzi wa Kina wa Uongezaji Thamani Madini Muhimu na Mkakati ya Tanzania (Manufacturing Africa – Critical Minerals Value Addition Study), katika hafla iliyofanyika jijini Dodoma

Akizungumza katika Mkutano huo uliohudhuriwa na Balozi wa Uingereza nchini Tanzania Mhe. Marianne Young akiongozana na maafisa wandamizi wa Ubalozi huo, wadau wa Sekta ya Madini, Wawekezaji, na wawakilishi, Waziri Mavunde alisema kuwa utafiti huo ni hatua muhimu katika kufanikisha azma ya Taifa ya kuyachakata madini muhimu na mkakati ndani ya nchi hadi kufikia bidhaa za mwisho kwa matumizi ya ndani na nje.


“Ni maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha tunaweka Mkakati kuyaongeza thamani madini muhimu yanayopatikana nchini hapa hapa ndani ya nchi. Dhamira ni kuyatumia madini yetu kama nyenzo ya kujenga uchumi wa viwanda na kupanua fursa za ajira na teknolojia,” amesema Waziri Mavunde. 


Waziri Mavunde alisisitiza kuwa, Tanzania imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi za madini muhimu kama vile nickel, graphite, rare earth elements, na lithium, madini ambayo ni mhimili wa teknolojia za kisasa, magari ya umeme, na nishati mbadala duniani.

“Kwa kuwekeza katika uongezaji thamani wa madini haya, tunajipanga kuwa kitovu cha uzalishaji wa malighafi ya kisasa kwa ajili ya soko la kimataifa,” amesisitiza Mavunde.


Aidha, Waziri Mavunde alieleza kuwa, Serikali imeweka mazingira rafiki kwa uwekezaji kwa kuboresha miundombinu, kujenga uwezo wa kitaalamu, na kuweka sera na motisha zinazowezesha uwekezaji katika mitambo ya uchenjuaji, uchenjuzi, na uzalishaji wa bidhaa za mwisho.


“Utafiti huu pia utaisaidia Serikali kutambua maeneo mahsusi ya kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya kuchakata madini, pamoja na fursa mpya za kiuchumi zitakazochochea maendeleo hapa nchini” ameongeza Mavunde. 

Kwa upande wake, Balozi wa Uingereza nchini Mhe. Marianne Young alisema kuwa taarifa hiyo ni sehemu ya ushirikiano baina ya mataifa hayo mawili (Tanzania na Uingereza) katika nyanja mbalimbali ikiwemo ya Sekta ya Madini ambao pia ameeleza Mkakati wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini ya Uingereza kushirikiana na GST kubadilishana uzoefu katika eneo la utafiti wa kina wa madini. 


Uchambuzi huo ni sehemu ya mpango mkubwa wa ushirikiano wa kimkakati wa Ushirikiano wa Ustawi wa Pamoja (Mutual Prosperity Partnership - MPP) kati ya Tanzania na Uingereza uliozinduliwa mwaka jana. Mpango huo pia unalenga kuvutia uwekezaji wa moja kwa moja kwenye Sekta ya Viwanda, hasa kwa kutumia madini muhimu/mkakati kama malighafi ya msingi.

Katika historia 2003 Ndipo Kundi hili la Wakilisha Lilipatikana.

 

WAKILISHA.

Mwaka 2002, kampuni ya vinywaji baridi ya Coca-Cola ilianzisha mradi wa kuibua vipaji vya muziki kupitia wasanii wanaochipukia nchini.


Kampuni hiyo ikaandaa Project ya vijana kushindana kuimba. Project hiyo ikapewa jina la “Coca-Cola Pop Idol”. Vijana mbalimbali wakajitokeza kushiriki.


Hatimaye Project ikapata mshindi. Msanii Banana Zorro akatangazwa kuwa kinara. Hata hivyo Banana alikuwa tayari ni 'Star' kutoka kundi la "B Love M" ikilinganishwa na washiriki wengine ambao hawakuwa wakijulikana.


Ushindi wa Banana ulitokana na kuimba kwa umahiri kibao "My Love" cha kundi la Westlife. Banana akakwea pipa kuzuru nchini Afrika Kusini katika ziara fupi ya kujifunza zaidi muziki.


Kanuni za shindano hilo zilieleza mapema kuwa mshindi wa kwanza atapata fursa ya kwenda nchini Afrika Kusini ili kunolewa kipaji chake. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa.


Ushindi wa Banana ukahamasisha vijana wengi mno kujitosa kushiriki msimu wa pili wa Project hiyo, ambao sasa ukapewa jina jipya la "Coca-Cola Pop Star", badala ya Coca-Cola Pop Idol, lililokuwa la mwanzo.


Mwanamuziki wa kundi la Kwaito la ‘'TKZee'’ kutoka Afrika Kusini, Zwai Bala, akafika nchini kwa mwaliko wa Coca-Cola kama Chief Judge, ili kusaidia Project hiyo kupata vipaji halisi katika msimu huo wa pili.


Hapa ndipo Coca-Cola Pop Star (2003) ikapata washindi watatu, ambao kanuni mpya za mashindano hayo zikahitaji waunde kundi moja litakalosafirishwa nchini Afrika Kusini ili kunolewa zaidi.


Washindi hao ni Langa Kileo, Sarah Kaisi na Witness Mwaijaga. Kundi lao likaitwa “Wakilisha” wakimaanisha wao ndiyo wawakilishi wa Kimataifa kutokea Tanzania katika project hiyo ambayo ilikuwa pia kwa nchi za Kenya na Uganda.


Ndani ya Wakilisha, Langa na Sarah walikuwa wachanga zaidi tofauti na Witness (Bad Gar) aliyekwishakuwa na msanii Florence Kasela (Dataz) kwenye kundi moja la Hip Hop liitwalo "The Dream Team".


"Wakilisha" wakawa moto haswa. Vibao vyao vya "Hoi" na "Kiswanglish" vikalipandisha chati kundi hilo ukanda wote wa Afrika Mashariki. Kila mtu akavutiwa na vijana hao kutoka Coca-Cola Pop Star.


Lakini kama ambavyo wahenga walisema kuwa 'Ivumayo Haidumu', ndivyo ilivyokuwa kwa "Wakilisha". Mafanikio ya kundi hili yakapelekea kupata msukosuko iliyoonesha dalili ya kundi hilo kufa siku si nyingi. 


Haiwi Ikawa, Msanii Sarah Kaisi (Shaa) akatangaza kujitoa kwenye kundi lao la Wakilisha na kufanya kundi hilo sasa kubakia na wasanii wawili tu, Langa Kileo na Witness Mwaijaga.


Kuondoka kwa Sarah (Shaa) Wakilisha, kukapelekea wasanii Langa na Witness kuondoa jina la "Sha" (Shaa) mbele ya jina la "Wakili-Sha", na sasa kundi lao kujulikana kama "Wakili" badala ya "Wakilisha".


Kuona hiyo haitoshi, "Wakili" wakatoa kibao kipya kiitwacho ‘No Chorus' wakilenga kumpiga dongo Sarah ambaye alikuwa mahiri zaidi kwa kuimba viitikio (Choruses) katika nyimbo za kundi hilo.


Kibao cha "No Chorus" kikaonekana kumshambulia Sarah kimtindo. Langa na Witness wakaimba kwenye wimbo huo kuwa wanasonga bila viitikio, na hakuna tatizo kwa wao kubaki wawili.


Biashara ya "Wakilisha" mpaka "Wakili" ikatamatika rasmi mwaka 2005. Langa na Witness wakaamua kuvunja kundi lao la kihistoria lililotokana na mradi wa kuibua vipaji wa Coca-Cola Pop Star.


Langa akapita kushoto, Witness akapita kulia. Kila mtu akageuka kujiangaikia yeye mwenyewe kama Solo Artist. Kifo rasmi cha "Wakilisha" kikawasikitisha wengi.


Enzi zikafika mwisho. 

Miaka miwili ikatosha kulilaza kwa amani kundi la "Wakilisha". Pumzika Langa Kileo. Kila la kheri kwenu Sarah na Witness. Ahsanteni kwa mchango wenu kwenye tasnia ya muziki.

#Balozi [0713 555 773]

Robert Prevost ni nani? Mfahamu kwa undani Papa mpya Leo XIV

 

Hata kabla jina lake halijatangazwa kutoka kwenye roshani ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, umati wa watu uliokuwa chini ulikuwa ukiimba "Viva il Papa" kwa maana ya Ishi milele Papa.

Robert Prevost, mwenye umri wa miaka 69, atakuwa kiongozi wa 267 kwenye kiti cha enzi cha Mtakatifu Petro na atajulikana kama Leo XIV.

Atakuwa Mmarekani wa kwanza kushika wadhifa wa Papa, ingawa anachukuliwa kuwa Kardinali kutoka Amerika ya Kusini kwa sababu ya miaka mingi aliyotumikia kama mmisionari nchini Peru, kabla ya kuwa askofu mkuu huko.

Ana uraia wa Peru na anakumbukwa kwa upendo kama mtu aliyefanya kazi na jamii zilizotengwa na kusaidia kuungfanisha jamii katika Kanisa la eneo hilo.

Alizaliwa Chicago mwaka 1955, Prevost alihudumu kama kijana wa altare na aliwekwa wakfu kuwa padri mwaka 1982.

Katika maneno yake ya kwanza kama Papa, Leo XIV alizungumza kwa upendo kuhusu mtangulizi wake Francis.

"Bado tunasikia masikioni mwetu sauti dhaifu lakini daima yenye ujasiri ya Papa Francis ambaye alitubariki," alisema.

"Tukiungana na kushikana mikono na Mungu, tusonge mbele pamoja," aliwaambia umati wa watu waliokuwa wakishangilia.

Aliwaambia umati uliokuwa ukisikiliza katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro kwamba alikuwa mwanachama wa Shirika la Augustino. Alikuwa na umri wa miaka 30 alipohamia Peru kama sehemu ya misheni ya Augustino.

Francis alimteua kuwa Askofu wa Chiclayo nchini Peru mwaka mmoja baada ya kuwa Papa.

Anawajua vizuri Makadinali kote ulimwenguni kwa sababu ya nafasi yake muhimu kama mkuu wa Baraza la Maaskofu.

Kwa kuwa asilimia 80 ya makadinali walioshiriki mkutano mkuu waliteuliwa na Francis, haishangazi sana kwamba mtu kama Prevost alichaguliwa.

Ataonekana kama mtu aliyeunga mkono kuendelea kwa mageuzi ya Francis katika Kanisa Katoliki.

Ingawa ni Mmarekani, na atakuwa anafahamu kikamilifu mgawanyiko ndani ya Kanisa Katoliki, historia yake ya Amerika ya Kusini pia inawakilisha mwendelezo baada ya Papa aliyetoka Argentina.

Ingawa wakati wake kama askofu mkuu nchini Peru hakuepuka kashfa za unyanyasaji wa kijinsia ambazo zimegubika Kanisa, jimbo lake lilikanusha vikali kwamba alihusika na jaribio lolote la kuficha ukweli.

Kabla ya mkutano mkuu, msemaji wa Vatican Matteo Bruni alisema kuwa wakati wa mikutano ya Baraza la Makadinali katika siku zilizotangulia mkutano mkuu walisisitiza umuhimu wa kuwa na Papa mwenye "roho ya kinabii inayoweza kuliongoza Kanisa ambalo halijifungi ndani bali linajua jinsi ya kwenda nje na kuleta mwanga kwa ulimwengu uliojaa kukata tamaa".

Kutoka BBC Swahili.

WATUMISHI SEKTA YA AFYA ZINGATIENI MAADILI YA KAZI ZENU – DKT. MAGEMBE


Na. WAF, Arusha

 

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amewataka watumishi wa sekta ya afya nchini kuzingatia maadili ya kazi zao na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

 

Dkt. Magembe ameyasema hayo Mei 8, 2025 jijini Arusha, wakati akizungumza na watumishi katika ziara yake ya kikazi Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Arusha Mount Meru.

 

Amesema kuwa kila mtumishi wa afya anatakiwa kufanya kazi kwa weledi  na  kuwa na mawasiliano mazuri baina yao na wagonjwa, ndugu wa wagonjwa pamoja na kuwa na lugha nzuri kwa wagonjwa wote wanaokwenda kupata huduma katika hospitali hiyo na kuongeza kuwa hatua za kisheria zichukuliwe kwa mtumishi atakayekwenda kinyume na kanuni na sheria za kiutumishi kwa kuwafikisha

kwenye mabaaraza ya kitaaluma.

 

“Ndio maana kuna Mabaraza ya Kitaaluma ambayo kazi yao kubwa ni kulinda taaluma na kuhakikisha maadili yanazingatiwa kinyume cha hapo ni kumchukulia hatua stahiki kwa mujibu wa sheria mtumishi anayekiuka maadili ya taaluma yake, ikumbukwe pia kila mtumishi wa afya alikula kiapo kuwa atawahudumia wananchi kwa nguvu zote na sio vinginevyo, hivyo tuyazingatie hayo na kufanya kazi kadri inavyopaswa na isitokee mwananchi amepoteza maisha kwa uzembe,” amesema Dkt. Magembe.

 

Aidha, Dkt. Magembe ameeleza kuwa Mkoa wa Arusha umejipambanua katika eneo la utalii na agenda ya Royal Tour imeubeba sana  mkoa huo hivyo ni vyema kuwahakikishia wananchi na watalii kiujumla wana uhakika wa matibabu pale wanapopata changamoto ya kiafya.

 

“Hospitali ya rufaa ya mkoa wa Arusha - Mount Meru imekuwa kimbilio kwa watalii wengi wanaokuja kwenye vivutio vilivyopo nchini pale wanapopata changamoto ya kiafya na hospitali ya Mount Meru imekuwa ikifanya vizuri na niwaombe muendelee hivyo ili muwe mfano wa kuigwa,”amesisitiza Dkt. Magembe.

Dkt. Magembe amewashukuru watumishi wote kwa kazi nzuri wanayofanya ya kuwahudumia wananchi na kusisitiza kuzingatia miiko, na maadili ya taaluma zao ili kutoa huduma bora kwa wananchi.

2004, Papa Leo XIV alifika nchini Tanzania

Mwaka 2004, Papa Leo XIV alifika nchini Tanzania na kufanya ziara kama Mkuu wa Shirika la Waagustiniani Ulimwenguni. 

Katika.ziara hiyo Papa Leo anayetoka katika Shirika la Order of Saint Augustine (OSA), alifika jijini Dar es Salaam kisha akaenda mkoani Njombe.

Ziara hiyo pia ilihusisha maeneo ya Mahanje hadi mkoani Songea.